PIA AMTETE MKUU WA MKOA PAUL MAKONDA Rais John Pombe Magufuli, akimpongeza Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Paul mak...
PIA AMTETE MKUU WA MKOA PAUL MAKONDA
Rais John Pombe Magufuli, akimpongeza Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Paul makonda, leo Machi 20, 2017 baada ya kutoa hotuba ya ukaribisho kwenye hafla ya uwekaji jiwe la msingi ujenzi wa Flyover Ubungo jijini Dar es Salaam. Kushoto ni Rais wa Benki ya Dunia, Dkt. Jim Yong Kim.
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzani Dkt. John Pombe Magufuli na Rais wa Benki ya Dunia Dkt. Jim Yong Kim wakifungua kitambaa ikiwa ni ishara ya kuweka jiwe la Msing la ujenzi wa barabara za juu (Interchange) kwenye makutano ya Ubungo March 20,2017.
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzani Dkt. John Pombe Magufuli na Rais wa Benki ya Dunia Dkt. Jim Yong Kim wakikata utepe ikiwa ni ishara ya kuanza kwa ujenzi wa barabara za juu (Interchange) kwenye makutano ya Ubungo March 20,2017.
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzani Dkt. John Pombe Magufuli na Rais wa Benki ya Dunia Dkt. Jim Yong Kim wakipata maelezo jinsi barabara za juu (Interchange) kwenye makutano ya Ubungo zitakavyokuwa baada ya kujengwa March 20,2017.
JAMHURI YA MUUNGANO WA TANZANIA
KURUGENZI YA MAWASILIANO YA RAIS IKULU
Simu: 255-22-2114512, 2116898
E-mail: press@ikulu.go.tz
Tovuti : www.ikulu.go.tz
Faksi: 255-22-2113425 |
OFISI YA RAIS,
IKULU,
1 BARABARA YA BARACK OBAMA,
11400 DAR ES SALAAM.
Tanzania.
|
TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. John Pombe Magufuli, leo tarehe 20 Machi, 2017 ameweka jiwe la msingi la ujenzi wa barabara za juu kwenye makutano ya barabara za Morogoro, Mandela na Sam Nujoma eneo la Ubungo Jijini Dar es Salaam (Ubungo Interchange).
Sherehe za kuweka jiwe la msingi katika mradi huo zimefanyika kando ya makutano ya barabara hizo na kuhudhuriwa na Rais wa Benki ya Dunia Mhe. Dkt. Jim Yong Kim, Mke wa Rais Mama Janeth Magufuli, Mawaziri wa Tanzania, Balozi wa China hapa nchini Mhe. Dkt. Lu Youqing, Mwenyekiti wa Kamati ya Bunge ya Miundombinu Mhe. Prof. Norman Sigala King na viongozi wengine wa Wizara na Mkoa wa Dar es Salaam wakiongozwa na Mkuu wa Mkoa huo Bw. Paul Makonda.
Ujenzi wa barabara hizo utagharimu Shilingi Bilioni 188.71 ambapo kati yake Shilingi Bilioni 186.725 ni mkopo wenye masharti nafuu kutoka Benki ya Dunia na Shilingi Bilioni 1.985 zitatolewa na Serikali ya Tanzania, na mradi huo utakaochukua muda wa miezi 30 unatekelezwa kwa lengo la kupunguza msongamano wa magari katika jiji la Dar es Salaam.
Akizungumza katika sherehe hizo, Rais wa Benki ya Dunia Mhe. Dkt. Jim Yong Kim amempongeza Mhe. Rais Magufuli kwa kazi nzuri anayofanya katika uongozi wake iliyomjengea sifa nzuri duniani kote.
“Nilivutiwa na hotuba za Mwalimu Julius Nyerere hasa aliposema bila uhuru hakuna maendeleo na bila maendeleo utapoteza uhuru wako, kwa maana hiyo Nyerere aliona kuwa maendeleo ndio njia pekee ya kulifanya Taifa kuwa imara na kujitawala na kuwawezesha watu kujua mwelekeo wa maisha yao.
“Nipo hapa kwa sababu viongozi wengi wa Afrika na wengine wengi duniani, wameniambia unatakiwa kwenda Tanzania, kuona kile anachofanya Rais Magufuli, ikiwemo kuzuia rushwa na kujenga uchumi wa nchi ambayo ni huru” amesema Dkt. Jim Yong Kim.
Kwa upande wake Mhe. Rais Magufuli ameishukuru Benki ya Dunia kwa kuunga mkono juhudi za maendeleo za Tanzania na ameahidi kuwa Tanzania itaendelea kushirikiana na benki hiyo kwa kuendelea kukopa na kulipa madeni yake.
Mhe. Dkt. Magufuli amesema ataendelea kutekeleza ahadi yake ya kukabiliana na msongamano wa magari katika Jiji la Dar es Salaam ambapo pamoja na kujengwa kwa barabara za juu katika makutano ya Ubungo, maandalizi yanaendelea kujenga njia ya barabara 6 za kuanzia Dar es Salaam hadi Chalinze Mkoani Pwani, kujenga kilometa 305 za reli ya kati kwa kiwango cha kisasa (Standard Gauge) kuanzia Dar es Salaam hadi Morogoro, kujenga bandari kavu katika eneo la Ruvu Mkoani Pwani na kujenga daraja la Salenda litakalounganisha Agha Khan na Coco Beach kupitia baharini.
Aidha, Mhe. Rais Magufuli ametoa wito kwa wananchi wa Dar es Salaam na Watanzania kwa ujumla kuunga mkono juhudi hizo nzuri na muhimu kwa maendeleo, na kuachana na ushabiki usio na manufaa unaochochewa na baadhi ya watu kupitia mitandao ya kijamii na baadhi ya vyombo vya habari.
Amewataka wakandarasi watakaojenga barabara za juu katika makutano ya Ubungo kuharakisha ujenzi huo, ikibidi kumaliza kabla ya miezi 30 na pia amewasihi wananchi watakaopata kazi katika mradi huo kuwa waaminifu na waadilifu wakati wote wa ujenzi.
“Tujielekeze katika masuala ya msingi na ya maendeleo, tuache kujielekeza katika udaku, tunapoteza muda mwingi katika masuala ambayo yanatupotezea muda” amesisitiza Mhe. Rais Magufuli.
Pamoja na kuweka jiwe la msingi Mhe. Dkt. John Pombe Magufuli na Mhe. Dkt. Jim Yong Kim wameshuhudia utiaji saini wa miradi 3 itakayopatiwa mkopo nafuu kutoka Benki ya Dunia ambayo ni mradi wa ujenzi wa miundombinu ya usafiri katika Jiji la Dar es Salaam, mradi wa kusambaza maji safi, mazingira na ukusanyaji wa maji taka, na mradi wa uendelezaji wa miji ya Arusha, Dodoma, Kigoma, Mbeya, Tanga, Mwanza na Mtwara, yote ikiwa na thamani ya Jumla ya Shilingi Trilioni 1.74.
Mhe. Rais Magufuli amesema pamoja na mkopo wa Shilingi Trilioni 1.74 Tanzania inatarajia kunufaika na mkopo mwingine wa Shilingi Trilioni 2.79 zitakazotumika katika miradi ya endelezaji bandari ya Dar es Salaam, umeme, gesi, kilimo, afya na elimu kwa Tanzania Bara na Zanzibar.
Gerson Msigwa
Mkurugenzi wa Mawasiliano ya Rais, IKULU
Dar es Salaam
20 Machi, 2017
COMMENTS