Na Gladness Mbisse wa Okanda Blog Mamlaka ya mapato Tanzania (TRA) imetoa semina kwa waandishi wa Mtandao kwa lengo la kukuza uelewa w...
Na Gladness Mbisse wa Okanda Blog
Mamlaka ya mapato Tanzania (TRA) imetoa semina kwa waandishi wa Mtandao kwa lengo la kukuza uelewa wao juu ya maswala ya ulipaji kodi pindi waandikapo habari hizo.
Semina hiyo ya siku moja iliyofanyika katika ukumbi wa BoT Dar es Salaam ambapo mamlaka hiyo imegundua umuhimu wa uwepo wa blogs nchini kwani wameonyesha kiu kubwa ya kutaka kuelewa maswala ulipaji kodi.
Akitoa mada katika semina hiyo mkurugenzi wa elimu na huduma kwa mlipa kodi, Richard Kayombo amesema ni vyema kushirikiana nao kwani watasaidia kufikisha elimu hiyo kwa jamii husika.
“ Tukiwa tunaelekea katika wiki ya elimu kwa mlipa kodi inayotarajiwa kuanza tarehe 4 mpaka 9 machi 2018 nchi nzima, tumeona ni vyema kuanza na kuwapa elimu waandishi hawa na kutusaidia kufikisha ujumbe kwani wakielewa wao jamii wanayoihudumia watapata habari iliyo sahihi” alisema.
Meneja wa Elimu kwa Mlipakodi wa Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) , Diana Masalla (aliyesimama mbele) akiwaelimisha baadhi ya Waandishi wa habari waliohudhuria Semina Maalum iliyohusu masuala ya kodi hususani katika matumizi ya mashine za Kielektriniki za kutolea Risiti (EfD), masuala ya utoaji taarifa ya fedha mpakani pamoja na masuala ya Wiki ya Elimu kwa Mlipakodi inayotarajiwa kuanza mapema tarehe 5 - 9 Machi, 2018.
Baadhi ya Waandishi wa habari waliohudhuria Semina iliyoandaliwa na Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) wakifuatilia uwasilishwaji wa mada toka kwa baadhi ya Watendaji wa Mamlaka hiyo (hawapo pichani) katika ukumbi wa Benki Kuu ya Tanzania (BoT), 3 Machi, 2018 Jijini Dar es Salaam.
Alifafanua kwamba wiki ya mlipa kodi hiyo ndiyo ya kwanza kufanyika kwa wakati mmoja nchi nzima ambapo kwa Dar es Salaam wilaya zote huduma hii itapatika.
“Tutakuwa na madawati ya kuwasikiliza wateja wetu kwa kila mkoa wa kodi yaani kwa Temeke tutakuwa ndani ya viwanja vya SabaSaba, Ilala tutakuwa katika ofisi zetu zilizopo Vingunguti, na Kinondoni wao watakuja TRA mwenge.”
Wiki hii ya mlipa kodi yenye kauli mbiu “KARIBU TUKUSIKILIZE NA UELIMIKE”wanamatarajio ya kukutana na wateja wote wenye kutatizwa na maswala yote yanayohusu ulipaji wa kodi kwani elimu hii bado inahitajika sana kwa watanzania walio wengi.
“Napenda kusisitiza tu kwamba tunaomba watoa risiti za mashine wa EFD watoe risiti zilizo sahihi na wateja pia wawe na tabia ya kudai risiti kila wanunuapo bidhaa.”alieleza Kayombo.
Kayombo amesema katika wiki hii maalumu ya mlipa kodi itajikita sana kutoa elimu katika Haki za mlipa kodi kwani unakuta mtu amefungua biashara anakuja kufanyiwa makadirio, bei anayoipata anaogopa kurudi tena TRA.
“Walipa kodi wengi wamekuwa wanalalamika wamekadiriwa kodi isiyo lakini Haki ya mlipa kodi inasema ukikadiriwa siyo mwisho wa dunia unatakiwa uende ukutane na meneja kama unaona umeonewa utoe vielelezo vyako tuone jinsi ya kuwekana sawa”.

COMMENTS