JAMHURI YA MUUNGANO WA TANZANIA WIZARA YA VIWANDA, BIASHARA NA UWEKEZAJI Simu Na-+255-22- 2129111/8 +255-22- 2...
JAMHURI YA MUUNGANO WA TANZANIA
WIZARA YA VIWANDA, BIASHARA NA UWEKEZAJI
Simu Na-+255-22- 2129111/8
+255-22- 2129109
Fax:+255-22-2125832
Website-www.mit.go.tz
|
NSSF Water Front, 1 Floor,
35 Edward Sokoine Road,
11469 DAR ES SALAAM.
|
TAARIFA KWA UMMA
Wizara ya Viwanda, Biashara na Uwekezaji inapenda kukanusha taarifa iliyotolewa katika mkutano uongozi wa CHADEMA na Wanahabari jana Jumatatu tarehe 31 Agosti, 2017 kuhusu suala la ubinafsishaji. Taarifa hiyo inakebehi uamuzi wa Serikali wa kuvirejesha Serikalini viwanda vilivyobinafsishwa na pia imedai kuwa hakuna viwanda vipya vilivyojengwa katika awamu hii kwa vile hamna mikopo ya kuanzisha viwanda.
Tunapenda umma utambue ukweli ufuatao:-
- Wakati wa ubinafsishaji wa viwanda, wawekezaji waliovichukua waliingia mikataba na Serikali ya kuviendeleza ili viendelee kuzalisha na hivyo kutoa ajira kwa wananchi na kuchangia mapato ya Serikali; ni kutokana na lengo hilo viwanda hivyo viliuzwa kwa bei ndogo.
- Siyo sahihi kujumuisha kuwa Serikali ina lengo la kuvirejesha viwanda vilivyobinafshishwa kwani kuna baadhi ya viwanda ambavyo wamiliki wake walitii masharti ya mikataba wakaviendeleza na kwa sasa vinatoa mchango mkubwa katika uchumi wa nchi. Viwanda hivi ni pamoja na kiwanda cha Bia (TBL), kiwanda cha Sigara (TCC), viwanda vya saruji (Mbeya Cement, Tanga Cement, Twiga Cement) n.k. Viwanda ambavyo Serikali inakusudia kuvirejesha serikalini ni vile ambavyo vilikiuka mikataba.
- Zoezi la ubinafsishaji wa viwanda lilifanyika kati ya mwaka 1990-1995. Kwa maneno mengine, ni zaidi ya miaka 20 imepita ambapo baadhi ya wamiliki hawajafanya juhudi yeyote ya kuviendeleza na hivyo kuviacha viwe magofu au kutumika kwa matumizi yasiyo na tija na ambayo ni kinyume na mikataba waliyoisaini. Hali hii haiwezi kuendelea kufumbiwa macho.
- Lengo la Serikali siyo kuvirejesha ili viendeshwe na Serikali, bali kuvitangaza kwa wawekezaji wenye uwezo wa kuviendeleza ili waendeleze uzalishaji ambao utatoa fursa ya kuwapa watanzania ajira na kuingiza mapato Serikalini.
- Ieleweke kuwa viwanda hivyo vilijengwa kwa fedha za watanzania, wakauziwa wawekezaji kwa mikataba ya kuviendeleza, na wao wakavunja mikataba hiyo kwa makusudi; kwa sababu hiyo, zoezi la kuvirejesha vile vilivyovunja mikataba halina ubaya wowote kama ilivyodaiwa na CHADEMA.
- Taarifa ya kutokuwepo na viwanda vipya katika awamu ya tano ati kwa vile hakuna mikopo ni ya kupotosha. Kwanza kabisa, si kweli kwamba hakuna mikopo inayotolewa katika kujenga viwanda. Ukweli ni kwamba kuna viwanda vilivyojengwa na vinavyoendelea kujengwa katika Awamu ya Tano kutokana na mikopo kutoka taasisi za kifedha za ndani. Mfano wa viwanda hivi ni Pipeline Industries; Global Packaging; Masasi Food Industries; CATA Mining Ltd nk. Pili, katika kuanzisha kiwanda siyo lazima mwekezaji akope fedha za ndani, kuna wawekezaji wengi ambao wanakuja na mitaji yao kutoka nje na wapo wawekezaji wa ndani ambao wanakopa nje na kujenga viwanda hapa nchini. Takwimu zinaonyesha kwamba katika kipindi cha Uongozi wa Awamu ya Tano, jumla ya viwanda vilivyosajiliwa na kuanza utekelezaji kupitia TIC ni 224, kupitia EPZA ni 41 na kupitia BRELA ni 128. Aidha, jumla ya viwanda vidogo na vya kati vilivyoanzishwa na Shirika la Viwanda Vidogo (SIDO) ni 2,143.
- Wizara ya Viwanda, Biashara na Uwekezaji inawatahadharisha wawekezaji waliobinafsishiwa viwanda na ambao hawajaviendeleza kuharakisha kufufua viwanda hivyo kwa mujibu wa mikataba yao, kwani zoezi la kuvirejesha viwanda hivyo serikalini limeanza kwa kasi. Aidha, Wizara inawashauri watanzania kuendelea kutumia fursa zilizopo kujenga viwanda ili tuharakishe kuipeleka nchi yetu katika uchumi wa kati kwa haraka.
Dkt. Adelhelm J. Meru
KATIBU MKUU – VIWANDA
WIZARA YA VIWANDA, BIASHARA NA UWEKEZAJI
01 Agosti, 2017
COMMENTS