WAZIRI MKUU Kassim Majaliwa ametoa wiki moja kwa Waziri wa Katiba na Sheria, Dk. Harrison Mwakyembe kumpa maelezo kuhusu sa...
WAZIRI
MKUU Kassim Majaliwa ametoa wiki moja kwa Waziri wa Katiba na Sheria,
Dk. Harrison Mwakyembe kumpa maelezo kuhusu sababu za Tanzania
kutokukamilisha mkataba wa Mawakili wa Afrika Mashariki kutambuana
katika utendaji wao.
Ametoa
agizo hilo leo (Ijumaa, Novemba 25, 2016) wakati akimuwakilisha Rais
Dk. John Magufuli katika ufunguzi wa mkutano wa 21 wa mwaka wa Chama cha
Wanasheria wa Afrika Mashariki kwenye Kituo cha Mikutano cha Kimataifa
cha Julius Nyerere (JNICC) jijini Dar es Salaam.
“Nimeshtushwa
kidogo kusikia kwenye taarifa yenu kuwa mkataba huo uliolenga nchi zote
za Afrika Mashariki hautaihusisha Tanzania kutokana na kutokukamilisha
sehemu yao ya kuufanyia kazi, nitahitaji maelezo,”
“Nitapenda
kupata maoni yako wewe mwenyewe Mheshimiwa Waziri wa Katiba na Sheria
wa Tanzania kwa vile wewe ni Mwanasheria mwandamizi na siyo
Mwanasheria wa Tanganyika Law Society peke yake kwa nini Tanzania
haijakamilisha mkataba huu,” amesisitiza.
Waziri
Mkuu amesema kwa mujibu wa maelezo ya awali aliyopewa kuhusu mkataba
huo, utakuwa na umuhimu mkubwa kwenye ukanda wa Afrika Mashariki kama
ilivyo kwenye sekta nyingine zinazoshirikiana ikiwemo uhandisi, uhasibu,
uthamini na uchoraji wa majengo.
Katika hatua nyingine Waziri
Mkuu amewataka Wanasheria hao kuzisaidia nchi zao ili ziondokane na
umaskini uliokithiri na Serikali zipate muda wa kushirikisha watu wake
katika kufanya kazi kwa lengo la kuwapatia maendeleo.
Amesema
nchi zilizoendelea na zinazoendelea, baada ya chaguzi hufanya shughuli
za ujenzi wa taifa lao na maendeleo ya watu wake. Ili kudumisha
demokrasia wana muda wa mikutano na maandamano na kazi.
“Hawaandamani
tu bila kupata kibali cha Polisi, hawaruhusiwi kuzuia magari yasipite,
kuzuia kazi isifanyike. Mfano kifungu cha 115 cha Sheria ya Taifa ya
Uchaguzi, kinataka kesi zinazotokana na uchaguzi ziwe zimefunguliwa
mahakamani ndani ya siku thelathini tangu kutangazwa kwa matokeo ya
uchaguzi na ziwe zimesikilizwa na kutolewa maamuzi ndani ya miezi kumi
na miwili tangu tarehe ya kufunguliwa mahakamani,” amesema..
Amesema
“kwa uelewa wa kawaida, Kifungu hiki ni kuwa jamii inataka masuala ya
siasa za uchaguzi yawe na muda wake wenye ukomo maalum ili baada ya hapo
wananchi waelekeze muda, nguvu na rasilimali zao nyingine katika kazi
au shughuli nyingine za maendeleo na ujenzi wa Taifa lao”.
Aidha,
Waziri Mkuu amesema eneo jingine ambalo ni muhimu kulitupia jicho ili
kukuza ushindani wa kibiashara katika Jumuia ya Afrika Mashariki ni la
uendeshaji wa mashauri mahakamani hasa kwa mashauri ya madai.
“Wote
tunakubaliana kuhusu misingi na haki za kidemokrasia kuwa kila mtu
anayo haki kikatiba na kisheria kusikilizwa madai yake na kutetea haki
zake; na kuwa chombo chenye mamlaka ya kutoa haki ni Mahakama”. Amesema.
Amesema
kuna taarifa za kuwepo kwa kesi zenye kuhusisha mali za thamani kubwa
zinazochukua muda mrefu sana kumalizika mahakamani huku baadhi ya sababu
za kuchelewa kwa kesi hizo ni utoaji wa maombi ya kuziahirisha mara kwa
mara kwa sababu binafsi jambo linalosababisha uendeshaji wa kesi kuwa
mgumu na kuchukua muda mrefu.
Waziri
Mkuu amesema wakati mwingine hata kesi zilizosikilizwa huendelea kubaki
mahakamani muda mrefu kutokana na maombi na rufaa za hapa na pale
zinazoishia kumnyima mwenye haki fursa ya kutekelezewa haki yake.
“Ni
wazi kesi kama hizi zinapohusisha mahusiano ya kibiashara na au mitaji
mikubwa ya biashara, matokeo yake ni kudumaza na hata kuua biashara,
achilia mbali ushindani wa kibiashara. Ni wajibu wenu Wanasheria kupata
ufumbuzi wa tatizo hili lenye athari hasi kibiashara,’ amesema.
Amesema
haki ya wadaiwa kusikilizwa kikamilifu na Mahakama, haki na uhuru
mlionao Mawakili kuwawakilisha wadaiwa wao bila hofu au shinikizo
lolote, viwe chachu ya maendeleo ya ushindani wa kibiashara na visiwe
kikwazo.
IMETOLEWA NA:
OFISI YA WAZIRI MKUU,
2 MTAA WA MAGOGONI,
S. L. P. 3021,
11410 DAR ES SALAAM.
IJUMAA, NOVEMBA 25, 2016.
COMMENTS