JAMHURI YA MUUNGANO WA TANZANIA WIZARA YA NISHATI NA MADINI Telegrams “NISHATI” Barabara ya Kikuyu, Simu: +02...
JAMHURI YA MUUNGANO WA TANZANIA
WIZARA YA NISHATI NA MADINI
Telegrams “NISHATI” Barabara ya Kikuyu,
Simu: +0262322018 S.L. P. 422,
Nukushi: 40474 DODOMA.
Barua pepe: info@mem.go.tz
TAARIFA KWA UMMA
TAARIFA KUHUSU WAKAZI WA MAHENGE NA LINDI KULIPWA FIDIA YA MRADI WA MADINI YA GRAPHITE (kinywe).
Tarehe 4 Julai, 2017, gazeti la Mtanzania katika ukurasa wake wa viii, liliandika habari yenye kichwa cha habari “Miradi ya kinywe Nachingwea, Ulanga yalipa fidia,”.
Mwandishi wa habari husika alimnukuu aliyekuwa Kaimu Kamishna wa Madini akisema kuwa “kwa kuzingatia umuhimu wa madini hayo, Serikali imeyapa kipaumbele na hivyo miradi ya Kinywe kule Mahenge na Lindi itaanza kutekelezwa na fidia imeanza kutolewa kwa wale wanaozunguka migodi tarajiwa kule Mahenge ambapo asilimia 80 ya waathirika wameshalipwa vilivyo,”
Aidha, aliyekuwa Kaimu Kamishna wa Madini alinukuliwa akisema kuwa wananchi wote walioathirika na uchimbaji wa madini hayo wilayani Nachingwea wamekwishalipwa ili kupisha uanzishwaji wa shughuli ya uchimbaji wa madini hayo.
Tunautaarifu Umma kuwa, aliyekuwa Kaimu Kamishna, hajawahi kuzungumza na chombo chochote cha habari kuhusu ulipaji wa fidia kwa wananchi wanaozunguka miradi hii.
Hivyo, tungependa kutoa taarifa sahihi kuwa, kwa Mradi wa Graphite wa Nachi-Ruangwa ambao unaendelezwa na Kampuni ya Uranex Tanzania, hatua iliyofikiwa ni kuwa, kati ya mali za watu 720 lilizothaminiwa, watu 668 tayari wamelipwa fidia ya jumla ya Sh.6.7 Bilioni.
Aidha, Watu 52 bado hawajachukua fedha zao na wakati wowote wakiwa tayari watazichukua. Watu 3 wamekataa kufanyiwa uthamini na Serikali inaendelea na mchakato wa kumaliza suala lao kwa mujibu wa sheria, kanuni na taratibu.
Kuhusu Mradi wa Graphite wa Mahenge unaoendelezwa na Kampuni ya TanzGraphite ambayo ni Kampuni Tanzu ya kampuni ya Kibaran Resources ya Australia, hatua iliyofikiwa ni kufanyika kwa uthamini wa mali ili wahusika waweze kulipwa fidia na kupisha eneo la mradi. Hadi sasa takriban asilimia 75 ya wahusika wamefanyiwa uthamini na elimu inaendelea kutolewa kwa wananchi wengine waliobaki ili wakubali kufanyiwa uthamini.
Hivyo, baada ya uthamini kukamilika na taarifa ya uthamini kuidhinishwa na Mthamini Mkuu wa Serikali ndipo malipo ya fidia yatafanyika.
Imetolewa na:-
Kitengo cha Mawasilino Serikalini
Wizara ya Nishati na Madini
Julai 10, 2017
COMMENTS