*Asema akishahamia, Mawaziri na Naibu Mawaziri wote wafuatie mara moja WAZIRI MKUU Kassim Majaliwa amesema atahamia Dodoma ifikap...
*Asema akishahamia, Mawaziri na Naibu Mawaziri wote wafuatie mara moja
WAZIRI MKUU Kassim Majaliwa amesema atahamia Dodoma ifikapo Septemba, mwaka
huu kuonyesha kuwa Serikali imedhamiria kutekeleza ahadi ilizotoa kwa wananchi.
Ametoa kauli hiyo leo asubuhi (Jumatatu, Julai 25, 2016) wakati akizungumza na mamia ya wakazi wa mkoa wa Dodoma na kuwashukuru kwa ushiriki wao kwenye maadhimisho ya Siku ya Kumbukumbu ya Mashujaa zilizofanyika kwenye uwanja wa Mashujaa, mjini Dodoma.
“Jana nilimwita Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu na kumwambia
akamilishe matengenezo kwenye nyumba yangu kwa sababu ninataka kuhamia Dodoma
ifikapo Septemba,” amesema na kushangiliwa na mamia ya wakazi wa mji wa Dodoma
waliohudhuria maadhimisho hayo.
Amesema tangu Serikali ya awamu ya tano iingie madarakani, kazi nyingi
zimefanyika na wananchi wameziona na kwamba sasa hivi kazi iliyobakia ni
utekelezaji wa ahadi alizotoa Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa
Tanzania, Dk. John Magufuli.
“Wananchi kazi mmeziona na sasa tunaenda kwenye utekelezaji. Ninatoa agizo
kuwa mawaziri na manaibu wote wahame mara moja kutoka Dar es Salaam na kuja
Dodoma. Wana ofisi ndogo Dodoma na kwa kuwa wamekuwa wakiishi wakati wote wa
Bunge, wahamie mara moja. Mimi nahamia Septemba, na utekelezaji wake
nitausimamia kwa juhudi zote,” alisisitiza.
Amewataka wakazi wa Dodoma watumie fursa hiyo kutunza amani ya nchi
na kudumisha umoja uliopo na pia akataka watumie fursa hiyo kujenga nyumba za
kuishi za kutosha, nyumba za kulala wageni na hoteli za kitalii ili watu
watumishi na wageni wanapokuja wasipate taabu mahali pa kuishi.
Wakati huo huo, mgeni rasmi kwenye maadhimisho hayo, Rais wa Jamhuri ya
Muungano wa Tanzania, Dk. John Magufuli katika muda wa siku tatu amerudia
kusisitiza nia ya Serikali kuhamia Dodoma katika kipindi chake cha
uongozi ili kutekeleza ndoto ya hayati Baba wa Taifa, Mwalimu Julius Kambarage
Nyerere ya kutaka makao makuu ya nchi yawe Dodoma.
Akizungumza na mamia ya wakazi wa mji wa Dodoma kwenye uwanja wa
mashujaa huku akishangiliwa, Rais Magufuli amesema atahakikisha Dodoma inakuwa
makao makuu ndani ya miaka minne na miezi minne iliyobakia kwenye awamu ya
kwnza ya uongozi wake.
“Kama wabunge karibu 300 na mawaziri na manaibu wao ambao hawafiki 30
wanakaa hapa kwa miezi mitatu na maisha yanakwenda, kama makao makuu ya chama
kinachotawala nchi yako hapa sioni sababu ni kwa nini Serikali ninayoiongoza
iendelee kubakia Dar es Salaam,” amesema.
Mara kwanza kutoa kauli hiyo, ilikuwa ni Jumamosi iliyopita, Julai
23, 2016 wakati akitoa hotuba yake ya kwanza mara baada ya kuchaguliwa kuwa
Mwenyekiti wa Chama cha Mapinduzi (CCM) na Mkutano Mkuu maalum wa chama hicho.
Rais Magufuli amesisitiza wananchi na wanasiasa kutunza amani na
kudumisha amani iliyokuwepo nchini. Pia amewataka Watanzania wote kuendelea
kuwaenzi mashujaa walioipigania nchi hii.
IMETOLEWA NA:
OFISI YA WAZIRI
MKUU,
S. L. P. 980,
DODOMA.
JUMATATU, JULAI 25, 2016.
Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa akiwasalimia wananchi wa Dodoma katika Maadhimisho ya Siku ya Kumbukumbu ya Mashujaa kwenye uwanja wa Mashujaa mjini Dodoma, Julai 25, 2016. |
Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa akiteta na Meya wa Manispaa ya Dodoma, Jafari Mwanyembwa katika Maadhimisho ya Siku ya Kumbukumbu ya Mashujaa kwenye uwanja wa Mashujaa mjini Dodoma, Julai 25, 2016. |
COMMENTS