Serikali imedhamiria kuwaunganisha wakulima wakubwa wa mazao ya chakula wa kata tano za Wilaya ya Iramba k...
Serikali imedhamiria
kuwaunganisha wakulima wakubwa wa mazao ya chakula wa kata tano za
Wilaya ya Iramba kwa kujenga daraja na makaravati manne katika barabara
yenye urefu wa kilomita 38.6 yatakayo gharimu shilingi bilioni 4.1.
Akiweka jiwe la msingi la ujenzi
wa daraja la Mto Mtoa na makaravati katika barabara ya
shelui-Mtoa-Urughu Kiongozi wa mbio za Mwenge wa Uhuru Amour Hamad Amour
amesema serikali imedhamiria kuwaunganisha wananchi ili wazalishe
mazao, waanzishe viwanda kisha kusafirisha bidhaa.
Amour amesema kwakuwa barabara
hiyo inahudumia wananchi wa kata za Shelui, Mtoa, Mtekente, Urughu na
Ndago wananchi wa maeneo hayo watumie fursa ya kuwa na barabara nzuri
kwa kutengeneza viwanda vidogo, vya kati na vikubwa na kisha kusafirisha
bidhaa na sio mazao kama mali ghafi.
Amesema kwa kufanya hivyo
wakulima wa mazao wataweza kujiongeza kipato chao kwa kuwa hawatapunjwa
kwa kuuzwa mali ghafi ambayo hupelekwa kwenye viwanda vya nchi nyingine
hivyo barabara hiyo iwe hamasa kwao kuzalisha kwa wingi pamoja na
kuanzisha viwanda kwa wingi.
Mradi huo wa barabara na
makaravati unatekelezwa kupitia mpango wa kuondoa vikwazo kwenye
barabara za vijijini, mpango unaofadhiliwa na serikali ya Tanzania kwa
kushirkiana na serikali za Uingereza na Ireland Kaskazini.
Kukamilika kwa ujenzi wa daraja
na makaravati hayo kutawezesha barabara hiyo kupitika kwa kipindi cha
mwaka mzima na hivyo kuwanufaisha wakazi elfu 79 wa kata hizo pamoja na
kuwezesha utoaji wa huduma za kijamii katika eneo hilo lenye shule za
msingi 29, shule za sekondari 6, zahanati 7 na kituo cha afya kimoja.
Wakati huo huo Kiongozi wa mbio
za mwenge wa Uhuru Amour Hamad Amour amezindua mradi wa ghala la
kuhifadhia chakula katika kijiji cha Nselembwe ambalo litakuwa
likihudumia jamii ya kata za Ulemo,Mgongo, Ntwike, Shelui na Mtoa.
Akifungua ghala hilo Amour
amesema kauli mbiu ya mwenge wa uhuru mwaka huu ni shiriki kukuza uchumi
wa viwanda kwa maendeleo ya taifa hivyo ujenzi wa ghala ili kuhifadhi
mazao unasaidia wananchi kutoyauza ovyo mazao na kuyahifadhi mahali
salama kabla ya kuyachakata kuwa bidhaa.
Amesema mradi huo wenye thamani
ya shilingi milioni 350 utaweza kuwasaidia wananchi kuhifadhi mazao kwa
mfumo wa stakabadhi ghalani na kuwa na kauli moja juu ya bei ya mazao
pia watakua na uhakika wa mazao.
Amour amewasisitiza wananchi wa
kata hizo kuzalisha kwa wingi kwa kuwa sasa wana uhakika wa sehemu
salama ya kutunzia mazao yao ili wasishawishike kuyauza kwa bei ndogo.
Mwenge wa Uhuru ukiwa Wilayani
Iramba umetembelea miradi yenye thamani ya shilingi bilioni 4.8 huku
ukipitia miradi 6 na kuona shughuli 5 katika vijiji 10 na tarafa 4
katika umbali wa km 119.1.
COMMENTS