Na Owen Mwandumbya, Bunge Spika wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Job Yustino Ndugai (Mb) amesema Bunge la...
Na Owen Mwandumbya, Bunge
Spika wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe.
Job Yustino Ndugai (Mb) amesema Bunge la Tanzania litaendelea kudumisha
mahusiano yaliyopo na Bunge Iran ili kubadilishana uzoefu katika maeneo
mbalimbali.
Mhe. Ndugai ameyasema hayo Mjini Dodoma leo
alipokutana na Balozi wa Jamhuri ya Kiislam ya Iran Nchini Tanzania Mhe.
Mohammad Dehghani aliefika Ofisini kwake Dodoma kwa ajili ya kuwasilisha salaam
na mualiko rasmi kutoka kwa Spika wa Bunge la Jamhuri ya Kiislam ya Iran
ukimualika Mheshimiwa ndugai kutembelea Bunge la Iran kwa lengo likiwa ni
kuimarisha uhusiano wa nchi zetu mbili.
Nashukuru kwa Salaam hizi
kutoka kwa Spika wa Bunge la Iran na naahidi kuzifikisha salaam hizi kwa
Waheshimiwa Wabunge na pia Ofisi yangu itatolea taarifa juu ya mwaliko huu na
kujipanga kutembelea Bunge la Irani kwa kadri muda utakavyoruhusu. Alisema Mhe. Ndugai
Pamoja na mwaliko huo wa Kibunge kutoka kwa Spika wa
Bunge la Iran, Balozi huyo Irani pia alitumia fursa hiyo kuwasilisha ombi la
Rais wa Iran Mhe. Hassan Rouhani la kumwalika Mhe. Ndugai ili aweze pia kuhudhuria Mkutano wa Kimataifa wa
kusaidia kutatua mgogoro wa muda mrefu kati ya Palestina na Israel uliopangwa kufanyika tarehe 22 Februari, 2017 Jijini
Tehran jambo ambalo pia aliahidi kulitolea majibu hivi karibuni.
Akizungumzia namna ya kuimarisha
mahusiano ya Mabunge haya mawili, Mhe. Ndugai alisisitiza umuhimu wa kuanzisha
Chama Rafiki cha Kibunge (Parliamentary
Friendship Group) baina ya Bunge la Tanzania na Bunge la Iran kwa kuwa kitasaidia
sana Wabunge wa Mabunge yote mawili kubadilishana uzoefu na kuimaisha uhusiano
uliodumu kwa muda mrefu baina ya Tanzania na Iran.
Kwa upande wa Mhe. Mohammad Dehghani
aliipongeza Tanzania kwa kuendelea kuimarisha demokrasia ambayo kwa kiasi
kikubwa nchi yake ya Iran imekuwa ikithamini na kuheshimu misingi imara
iliyowekwa na Baba wa Taifa Hayati Mwl. Julius Kambarage Nyerere.
Nchi yenu imekuwa na historia kubwa
sana ya kimahusiano na Iran, pamoja na mambo yote napongeza sana jitihada
mnazozichukua kuimarisha demokrasia ikiwa ni pamoja na kuongeza idadi ya
Wabunge wanawake Bungeni na nimatumaini yetu kuwa mtayafikia malengo mliyojiwekea
ya kufikia idadi ya 50 kwa 50. Alisema Bolozi Dehghani
Awali, akimkaribisha mgeni wake, Mhe. Ndugai
alimshukuru Mhe. Balozi kwa kutenga muda na kusafiri kutoka Jijini Dar es
Salaam kuja Dodoma ambapo pia alitumia nafasi hiyo kumpa pole Mhe. Balozi kwa
matukio mawili makubwa yaliyoikumba nchi ya Iran hivi karibuni.
“Mhe. Balozi, kabla ya yote kwa niaba ya Bunge la
Tanzania natoa pole kwa msiba mkubwa wa kifo cha Rais wa Nne wa Iran Hayati
Akbar Hashemi Rafsanjani kilichotokea taehe 08 Januari, 2017 na pili ni tukio
la kuanguka kwa jengo kubwa la kibiashara Jijini Tehran lililosababisha vifo
vya watu ishirini (20) na majeruhi zaidi ya 200, tarehe 19 Januari, 2017”. Alisema
Mhe. Ndugai
COMMENTS