Na Bahati Mollel-TAA, Iringa TIMU ya Uchukuzi jana ilijizolea vikombe saba baada ya wachezaji wake kuibuka mabingwa na washindi wa tat...
Na Bahati Mollel-TAA, Iringa
TIMU ya Uchukuzi jana ilijizolea vikombe saba baada ya wachezaji wake kuibuka mabingwa na washindi wa tatu katika michuano ya Kombe la Mei Mosi kwenye michezo ya riadha, karata, bao na draft iliyofanyika kwenye uwanja wa Samora na ukumbi wa Manispaa Iringa.
Nyota njema ilianza kuonekana alfajiri kwa Uchukuzi baada ya wanariadha wake Scolastica Hasiri kushinda mbio za kilometa nane kwa wanawake baada ya kutumia dakika 46:16 huku Colnel Kufahaidhuru ameshika nafasi ya tatu kwa wanaume baada ya kutumia dakika 44:01 zikiwa ni mbio za kilometa 10.
Ushindi wa pili wa riadha kwa wanawake umechukuliwa na Cartace Manampo wa Shirika la Umeme Tanzania (Tanesco) kwa kutumia dakika 46:50 na mshindi wa tatu ni Sophia Komba wa Ofisi ya Rais Ikulu amtumia dakika 51:46.
Kwa upande wa wanaume katika mchezo wa riadha bingwa ni Lazaro Lugano Shirika la Umeme Tanzania (Tanesco) ametumia dakika 42:28, huku mshindi wa pili ni Michael Luanga wa Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) alitumia dakika 43:20.
Nafasi ya nne imekwenda kwa Francis Sweetbert wa Ofisi ya Taifa ya Ukaguzi wa Hesabu (NAO) kwa muda dakika 45:18, huku wa tano ni Hakim Ambari wa Ofisi ya Rais Ikulu alitumia dakika 47:10 na wa mwisho ni Shaaban Kidang’ala wa Mamlaka ya Hifadhi ya Ngorongoro (NCAA) alitumia dakika 57:46.
Katika mchezo wa draft wanawake Neema Makassy wa Uchukuzi ameibuka bingwa baada ya kujikusanyia pointi 10, akifuatiwa na Rosemary Skainda wa Ofisi ya Taifa ya Ukaguzi wa Hesabu (NAO) mwenye pointi sita; naye Rebecca Chaula wa MUHAS amekuwa mshindi wa tatu kwa kujikusanyia pointi nne.
Kwa upande wa wanaume mchezo wa draft mchezaji Johnson Ngido wa Uchukuzi ameibuka bingwa, akifuatiwa na Alphonce Sika wa Ofisi ys Taifa ya Ukaguzi wa Hesabu (NAO) na mshindi wa tatu ni Joseph Mlimi wa Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA).
Katika mchezo wa karata wanaume ubingwa umechukuliwa na mchezaji Wilhemin Bayanga wa Geita Gold Mine (GGM), huku mshindi wa pili ni Nkwabi Kagado wa Shirika la Umeme Tanzania (Tanesco) na wa tatu ni Moses Machunda wa Uchukuzi. Kwa upande wa wanawake Emily Kyando wa MUHAS ameibuka mshindi, akifuatiwa na Sheila Mwihava wa Tanesco na Zamaradi Yussuf wa Uchukuzi akiwa tatu.
Katika mchezo wa bao wanawake Sharifa Amir, wa pili ni Jacky Massawe wa Tanesco na watatu ni Severina wa MUHAS.
Michuano hiyo inaendelea leo kwa timu ya Shirika la Umeme Tanzania (Tanesco) kuumana na Mamlaka ya Hifadhi ya Ngorongoro (NCAA) katika mchezo wa netiboli, wakati katika kamba wanaume Uchukuzi watavuta na Tanesco; huku NCAA watacheza na NAO.
Mchezaji Neema Makassy wa Uchukuzi (kulia) akichuana na Rebecca Chaule wa MUHAS katika mchezo wa draft kwa wanawake wa michuano ya Kombe la Mei Mosi uliofanyika kwenye ukumbi wa Manispaa Iringa.
|
COMMENTS