Na Mwandishi Wetu Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano Profesa Makame Mbarawa, ameitaka Mamlaka ya Usafiri wa Anga Tanzania (TCAA...
Na Mwandishi Wetu
Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na
Mawasiliano Profesa Makame Mbarawa, ameitaka Mamlaka ya Usafiri wa Anga
Tanzania (TCAA), kusimamia usafiri wa anga kwa kuzingatia taratibu na kanuni za
usafiri huo ili kuweka uwiano wa haki kwa waendeshaji na abiria wanaotumia
usafiri huo.
Ametoa kauli hiyo mjini Dodoma wakati
akizindua rasmi Baraza la Wafanyakazi wa Mamlaka hiyo na kuwapongeza kwa kuamua
kuweka mikakati ya kununua rada nne kwa kutumia fedha za ndani.
“Lazima msimamie kanuni na taratibu
zilizopo, wajibu wenu ni kutoa haki kwa watumiaji na abiria kwa usawa, hatutaki
kusikia mnakandamiza watumiaji wa usafiri na mkisimamia vizuri eneo hili
mtafanya idadi ya watumiaji kuongezeka na makampuni kuendelea kuwekeza zaidi
kwenye usafiri” amesisitiza Prof. Mbarawa.
Waziri Prof. Mbarawa amesema yeyote
anaevunja taratibu zilizowekwa kwenye usafiri wa anga Mamlaka hiyo ichukue
hatua stahiki kulingana na taratibu zilizopo ili usafiri huo uweze kuwa na
nidhamu.
“Kila Kampuni mkiiachia ifanye
inavyotaka hatutafika popote na malalamiko kwenye usafiri wa anga yataendelea
kuwepo, hivyo naomba msimamie makampuni haya kwa ukaribu mkubwa,’ amesisitiza
Prof. Mbarawa.
Ameongeza kuwa ili mamlaka ifikie
lengo na kufanikiwa lazima Menejimenti ishirikishe watumishi kwa karibu ili
kutimiza malengo iliyojiwekea.
Prof. Mbarawa amesisitiza umuhimu wa TCAA
kuwawezesha watumishi wake kitaaluma na kimaslahi ili kuongeza tija katika kazi
na kufikia malengo ya utendaji Kitaifa na Kimataifa.
Kwa upande wake Mkurugenzi Mkuu wa
Mamlaka hiyo, Bw, Hamza Johari, amemhakikishia Waziri Prof. Mbarawa kuwa TCAA
imejipanga kutekeleza miradi mbalimbali kwa kutumia vyanzo vya ndani ili
kuvutia makampuni ya ndege ya ndani na nje ya nchi.
“Nikuhakikishie kuwa tumejipanga kutekeleza
miradi mingi zaidi kwenye usafiri wa ndani ili kuchochea kasi ya usafiri huo
lakini pia kutimiza amza ya kuboresha usafiri huo, ”amesema Johari.
Ameongeza kuwa kwa sasa mamlaka iko
kwenye hatua za awali za utekelezaji wa mradi wa kufunga vifaa maalum vya
kuwezesha ndege kwa usalama katika Kiwanja cha Ndege cha Kimataifa cha Zanzibar
ambapo mradi huo ukikamilika utaimarisha huduma za kuongozea ndege katika
kiwanja hicho.
IMETOLEWA NA KITENGO CHA HABARI NA
MAWASILIANO WIZARA YA UJENZI, UCHUKUZI, MAWASILIANO.
Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, Profesa Makame Mbarawa katika picha ya pamoja na Wajumbe wa Baraza la Mamlaka ya Usafiri wa Anga Tanzania (TCAA) lililofanyika mjini Dodoma.
|
COMMENTS