Mbunge wa Kigoma Mjini Mheshimiwa Zitto Kabwe (mbele), akimsikiliza mwenyekiti wa Kamati ya Bunge ya Haki, Kinga na Madaraka ya Bunge leo Se...
Mbunge wa Kigoma Mjini Mheshimiwa Zitto Kabwe (mbele), akimsikiliza mwenyekiti wa Kamati ya Bunge ya Haki, Kinga na Madaraka ya Bunge leo Septemba 21, 2017 mjini Dodoma. Mheshimiwa Zitto ambaye pia ni Kiongozi wa chama cha ACT-Wazalendo, amefikishwa mbele ya kamati hiyo ikiwa ni siku moja baada ya kukamatwa kwenye uwanja wa ndege wa Kimataifa wa Julius Nyerere akitokea mkoani Kigoma Septemba 20, 2017, kufuatia agizo la Spika wa bunge Mheshimia Job Ndugai, ambaye aliagiza Mbunge huyo kufika mbele ya kamati hiyo kufutia maandishi yake aliyoyachapisha kwenye akaunti yake ya Tweeter na mitandao mingine ya kijamii ambayo Spika alisema yamelidharau bunge.(Picha Ofisi ya Bunge)
Kamati ya Bunge ya Haki, Maadili na Madaraka ya Bunge, leo imemuhoji Mbunge Kigoma Mjini Zitto kufuatia agizo la Mheshimiwa Spika la kumtaka Mbunge huyo ahojiwe kutokana na kauli mbalimbali alizozitoa za kulidharau Bunge.
Zitto alifika mbele ya Kamati hiyo majira ya saa 9 alasiri na kuhojiwa kwa takribani saa tatu.
Akizungumzia kikao hicho, Mwenyekiti wa Kamati ya Haki, Maadili na Madaraka ya Bunge, Mhe. Kapteni Mstaafu George Mkuchika alisema Kamati imesikiliza maelezo ya Mhe. Zitto kuhusiana na tuhuma ambazo zilikuwa zinamkabili.
“Kamati imemhoji Mheshimiwa Zitto amejibu maswali yote aliyotakiwa kuyajibu, Kamati imemaliza kazi yake na kwa mujibu wa utaratibu uliopo ikimaliza kazi inaanda Ripoti na kuipeleka kwa Mheshimiwa Spika,” ,” alisema.
Akizungumzia sababu za Zitto kupelekwa mbele ya Kamati hiyo chini ya ulinzi wa Jeshi la Polisli alisema kwa mujibu wa Sheria ya Kinga, Haki na Madaraka ya Bunge mtu anayeitwa mbele ya Kamati ya Haki, Maadili na Madaraka ya Bunge hupelekewa Hati ya Kuitwa na Katibu wa Bunge.
“Kutokana na kwamba hakufika na hakukuwa mawasiliano yoyote, Sheria inaruhusu Mhe. Spika kutoa Hati ya kukamatwa na kuletwa kwenye kikao cha Kamati,” alisema.
Alisema Mhe. Zitto alipewa Hati ya kuitwa Septemba 13 kwa ajili ya kufika mbele ya Kamati kesho yake Septemba 14 lakini hakufika na hakutoa taarifa ndio maana akapelekwa pale chini ya ulinzi wa polisi.
Septemba 12, mwaka huu, Mhe. Spika Job Ndugai aliagiza Mbunge huyo kufika mbele ya kamati hiyo kwa ajili ya kuhojiwa kuhusiana na kauli zake alizozitoa kwenye mitandao ya kijamii kwamba Mhimili wa Bunge umewekwa mfukoni na Serikali na kwamba Bunge lilikosea kushughulikia Taarifa za Kamati kuhusu Almasi na Tanzanite.
COMMENTS