Mmoja ya watumishi wa iliyokuwa Mamlaka ya Ustawishaji Makao Makuu Dodoma akiuliza swali kwa ...
Mmoja
ya watumishi wa iliyokuwa Mamlaka ya Ustawishaji Makao Makuu Dodoma
akiuliza swali kwa Waziri wa Nchi ya Ofisi ya Rais TAMISEMI George
Simbachawene (hayupo pichani) wakati wa mkutano na Waziri huyo jana
katika ukumbi wa Shule ya Sekondari ya Dodoma. PICHA NA BERN PATRICK
……………………………………………………………..
NA RAMADHANI JUMA
OFISI YA MKURUGENZI-MANISPAA DODOMA.
SERIKALI imewapangia vituo vipya
vya kazi watumishi 260 wa iliyokuwa Mamlaka ya Ustawishaji Makao Makuu
Dodoma (CDA) baada ya Mamlaka hiyo kuvunjwa na Rais wa Jamhuri ya
Muungano wa Tanzania Dokta John Magufuli Mei 15 mwaka huu.
Rais Dokta Magufuli alilazimika
kuivunja Mamlaka hiyo ili kuondoa mkanganyiko wa kimajukumu kati ya
Mamlaka hiyo na Halmashauri ya Manispaa ya Dodoma hususan katika masuala
ya umilikishaji wa ardhi.
Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais
TAMISEMI George Simbachawene alikutana na watumishi hao wakati wa ziara
yake katika Halmashauri ya Manispaa ya Dodoma jana na kuwasomea vituo
walivyopangiwa katika taasisi mbalimbali za serikali.
Kwa kujibu wa Waziri
Simbachawene, watumishi 150 wamehamishiwa katika Halmashauri ya Manispaa
ya Dodoma, idadi ambayo ni zaidi ya nusu ya watumishi wote 260.
Watumishi 66 wamepangwa katika
Mikoa na Wilaya mbalimbali Nchini, watumishi 16 wamehamishiwa katika
Ofisi ya Rais TAMISEMI, mtumishi mmoja amepangwa katika Ofisi ya Rais
Utumishi, na watumishi watatu wamehamishiwa Chuo Kikuu cha Dodoma
(UDOM).
Taasisi zingine ni Ofisi ya
Waziri Mkuu ambayo imepangiwa watumishi watatu, Wizara ya Ardhi
watumishi wawili, Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania limepangiwa
mtumishi mmoja, watumishi wanne wamehamishiwa katika Hospitali ya
Benjamin Mkapa iliyopo Manispaa ya Dodoma na watumishi 14 wamehamishiwa
katika kampuni inayosimamia mradi wa mabasi ya mwendo kasi jijini Dar es
Salaam (DART).
Kwa Mujibu wa Waziri
Simbachawene, Watumishi wote waliopangiwa katika Mamlaka za Serikali za
Mitaa watakuwa wameshakabidhiwa barua zao za Uhamisho kufikia Julai 12
mwaka huu, ambapo wale waliopangiwa Serikali Kuu watakabidhiwa barua zao
muda wowote kuanza sasa kabla ya kuripoti katika vituo vyao vipya vya
kazi na kuendelea na majukumu watakayopangiwa.
COMMENTS