SERIKALI imemuagiza Meneja wa Uwanja wa Ndege wa Mpanda kuwasiliana na Kampuni ya Uendelezaji Uwanja wa Ndege wa Kilimanjar...
SERIKALI
imemuagiza Meneja wa Uwanja wa Ndege wa Mpanda kuwasiliana na Kampuni ya
Uendelezaji Uwanja wa Ndege wa Kilimanjaro
(KADCO) ili kupata gari la Zimamoto ili ndege za Shirika la ndege Tanzania
(ATCL) ziweze kuanzisha safari zake katika Mkoa wa Katavi.
Akizungumza
mara baada ya kukagua uwanja huo Naibu Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na
Mawasiliano, Eng. Edwin Ngonyani amesema kwa muda sasa kiwanja hicho kimekuwa
kikitumiwa na ndege chache za Shirika la
kuhudumia wakimbizi (UNHCR), hivyo ni wakati sasa kutumika na ndege zetu ili kuboresha
huduma za usafiri wa anga Mkoani hapa.
“Kamilisheni
mazungumzo na KADCO ili kupata gari la
Zimamoto lenye ujazo wa Lita 4,000 litakalokuwa na uwezo wa kukabiliana na majanga
ya moto endapo yatatokea, kutakapokuwa na gari hilo uwanjani hapa tutaanzisha
safari za ndege za Shirika letu wakati ndege yetu ta tatu itakapowasili,”
amesema Eng. Ngonyani.
Aidha,
amemtaka meneja wa Uwanja huo wa ndege kuhakikisha anaingiza uwanja huo katika
mpango maalum kwa ajili ya ujenzi wa taa kiwanjani hapo ili uwanja huo uweze
kutumika kwa mchana na usiku.
Eng.
Ngonyani ameongeza kuwa azima ya Serikali ni kuhakikisha usafiri wa anga nchini
unaimarika kwa kutumia ATCL na mashirika
mengine yalipo nchini hivyo kama Serikali imejipanga kuendelea kuboresha
miundombinu ya viwanja ili viwe katika viwango vinavyokubalika.
Kwa
upande wake Meneja wa Uwanja huo Seneth Lyatuu amemuhakikishia Eng. Ngonyani
kuwa changamoto ya kuwa na Gari la zimamoto itatatuliwa mapema ili wakazi wa
Mpanda waweze kunufaika na huduma za ATCL na hivyo kuwapa unafuu watumiaji wa usafiri wa anga.
“Kuanza
kwa safari za ATCL hapa Mpanda kutawapunguzia gharama wananchi ambao kwa sasa
hulazimika kwenda Mwanza au Mbeya ili kupata ndege ya kwenda Dar es Salaam na
gharama huwa kubwa,” amesisitiza Lyatuu.
Naye
Mkuu wa Wilaya ya Tanganyika Bw. Saleh Mhando
amesema kutalete tija na kutafungua fursa ya utalii wa ndani na nnje ya
nchi hasa kwa kuwepo na Mbuga ya Katavi ambayo ina vivutio vingi.
Katika
hatua nyingine Eng. Ngonyani amelipongeza Shirika la Reli Tanzania (TRL) kwa
kutekeleza agizo la Serikali la kutumia Mfumo wa kielektroniki katika kudhibiti
mapato ambapo shirika hilo limeanza kukatisha tiketi kwa njia hiyo katika stesheni
za Mpanda na Tabora.
Imetolewa na Kitengo
cha Mawasiliano Serikalini, Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano.
Naibu
Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano Eng. Edwin Ngonyani(Kulia) akikagua
Mfumo wa ukatishaji tiketi kwa njia ya kielekroniki katika Stesheni ya Mpanda
Mkoani Katavi. Katikati ni Meneja Mradi wa kampuni ya Makgroup Ltd Bw. Joseph
Mrosso.
Naibu
Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano Eng. Edwin Ngonyani (Kushoto) akipata
maelezo kutoka kwa Meneja wa Kampuni ya Reli Tanzania, Kanda ya Tabora Bw.
Frederick Masangwa(Katikati), wakati alipokagua huduma za usafiri wa Reli
Mkoani Katavi.
Meneja
wa Msimamizi wa Bandari ya Kigoma Bw. Morris Mchindiuza (aliyenyoosha mkono)
akimwonesha Naibu Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano Eng. Edwin Ngonyani
(Wa pili kulia) eneo itakapojengwa bandari ya Kalema iliyopo Wilaya ya
Tanganyika Mkoani Katavi.
Naibu
Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano Eng. Edwin Ngonyani (Wa pili) akitoka
kukagua kingo za bandari ya Kalema iliyopo Wilaya ya Tanganyika Mkoani Katavi
COMMENTS