Na Shamimu Nyaki-WHUSM. Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Mama Samia Suluhu Hassan jana ameongoza Watanzania na w...
Na Shamimu Nyaki-WHUSM.
Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Mama Samia Suluhu Hassan jana ameongoza Watanzania na wapenzi wa mpira wa miguu nchini kushuhudia mechi ya kirafiki kati ya timu ya Everton ya Uingereza na Gor Mahia kutoka Kenya Uwanja wa Taifa Jijini Dar es Salaam.
Mchezo huo ulihudhuriwa na Viongozi wa mbalimbali wa Kitaifa wakiwemo Marais wastaafu Mhe. Alhaj Alli Hassan Mwinyi na Mhe. Jakaya Mrisho Kikwete, Balozi wa Uingereza nchini Bibi. Sarah Coker pamoja na viongozi wengine.
Katika mchezo huo uliochezwa zaidi ya dakika 90 timu ya Everton iliibuka mshindi wa magoli mawili dhidi ya goli moja la Gor Mahia. Goli la kwanza la Everton likifungwa na nyota wake Wayne Rooney katika dakika ya 34 kipindi cha kwanza na baadaye timu ya Gor Mahia iliweza kusawazisha katika dakika ya 37 kupitia mchezaji wake Tuyisenge Jacquer.
Katika Kipindi cha pili, timu zote zililirudi kwa kasi zikionyesha mbinu mbalimbali za kuukabili mpira na dakika ya 71 Everton ilijipatia goli la pili kupitia mchezaji wake Kierdin Dowell na hivyo kuibuka washindi dhidi ya Gor Mahia kwa magoli 2-1.
Mechi hiyo ilikuwa ya kirafiki yenye lengo la kuimarisha timu zao pamoja na mahusiano katika sekta ya michezo katika nchi za Uingereza na Afrika Mashariki iliyoandaliwa na Kampuni ya SportPesa ikiwa ni maandalizi ya msimu mpya wa ligi kwa mwaka 2017/2018 kwa mataifa mbalimbali duniani.
Wachezaji wa timu ya Everton ya England na Gor Mahia ya Kenya wakiwa uwanjani jana Jijini Dar es Salaam. |
COMMENTS