NA MWANDISHI WETU, SIMIYU BENKI ya Maendeleo ya Kilimo Tanzania (TADB) imeuhakikishia uongozi wa Mkoa wa Simiyu kuwa itafanya...
NA MWANDISHI WETU, SIMIYU
BENKI ya Maendeleo ya Kilimo Tanzania (TADB)
imeuhakikishia uongozi wa Mkoa wa Simiyu kuwa itafanya kazi kwa karibu katika
kutoa fursa ya mikopo itakayowasaidia wakulima mkoani humo kulima kilimo
chenye tija.
Akizungumza na Mkuu wa Mkoa wa Simiyu Anthony Mtaka pamoja na Wakurugenzi na Wataalam
kilimo na umwagiliaji, ushirika na mifugo kutoka Halmashauri zote za
Simiyu,Kaimu Mkurugenzi wa Banki hiyo Francis Assenga(pichani juu)
amesema wapo tayari kukopesha na kufanya kazi na Mkoa wa Simiyu kutokana
na utayari wao na uwepo wa mwongozo elekezi wa shughuli za kilimo zilizofanyiwa utafiti.
Amesema Benki hiyo ambayo ina lengo
la kuleta mapinduzi ya kilimo Tanzania imeridhia kutoa mikopo katika miradi ya kilimo kwa wakulima, vikundi
vilivyosajiliwa, vyama vya ushirika na kupitia Benki na taasisi nyingine za kifedha
ambazo zinaweza kuwakopesha wakulima, ili kukuza uchumi na kupunguza umaskini kwa wakulima mkoani humo.
Ameongeza kuwa ili kufanikisha azma ya
Mkoa wa Simiyu ya kukifanya kilimo kuwa ni biashara na kukuza uchumi wa
wakulima wake , Benki ya TADB itasaidia kutoa mikopo itakayoambatana na
mafunzo ya kuwajengea uwezo wakopaji hususani wanawake na vijana.
Ameeleza kuwa benki yake imekwisha tenga kiasi cha shilingi milioni 650 kwa ajili ya
mafunzo ya kuwajengea uwezo na Bil 42 za mkopo kwa wanawake na vijana, hivyo
amezisisitiza Halmashauri za Mkoa wa Simiyu kuwahamasisha vikundi vya wakulima
vilivyosajiliwa kuchangamkia fursa hiyo ya mikopo yenye riba ndogo na masharti
nafuu.
Mkuu wa Mkoa wa Simiyu , Mhe. Anthony
Mtaka amesema Mkoa wa Simiyu uko tayari kufanya kazi na Benki ya TADB kupitia
vikundi vya uzalishaji, Halmashauri na Miradi mbalimbali inayotekelezwa mkoani
humo, ikiwa ni pamoja na miradi ya umwagiliaji ya Mwamanyili Wilayani
Busega ulio katika hatua ya upembuzi yakinifu na Mwasubuya wilayani Bariadi
ambao uko katika hatua ya ujenzi wa miundombinu ya umwagiliaji.
“Tungehitaji kuwa Mkoa ambao kupitia
Benki ya Maendeleo ya Kilimo tungetengeneza namna ambayo ingewasaidia wakulima
na ikasaidia mikoa mingine kuja kuona maendeleo ya kilimo ambayo ni matokeo
ya Serikali kuwekeza katika Benki ya Kilimo” amesema Mtaka.
"Sisi kama Mkoa tumejipanga,
tumetoa Elimu ya utayari na
namna ya utekelezaji wa shughuli zote kwa wataalam wetu pamoja na wananchi na isitoshe tayari tumeshafanya utafiti na kuandaa mwongozo wa uwekezaji ndani ya mkoa, hivyo tunawakaribisha kuwekeza,” Amesema Mtaka.
namna ya utekelezaji wa shughuli zote kwa wataalam wetu pamoja na wananchi na isitoshe tayari tumeshafanya utafiti na kuandaa mwongozo wa uwekezaji ndani ya mkoa, hivyo tunawakaribisha kuwekeza,” Amesema Mtaka.
Aidha Mtaka ameongeza kuwa Mkoa wa
Simiyu unatekeleza Sera ya Uchumi wa Viwanda chini ya Kauli Mbiu ya “Wilaya
Moja Bidhaa Moja Kiwanda Kimoja” ambapo hadi sasa kuna kiwanda cha chaki na maziwa na
miradi mingine minne ya viwanda iko katika upembuzi yakinifu, hivyo benki
inaweza kuwekeza katika miradi hii kwa kuwawezesha wakulima na wafugaji
kuzalisha malighafi ya Viwanda hivyo au kuwa mdau katika viwanda hivyo.
Naye Mkurugenzi wa Biashara na Mikopo wa
TADB Augustino Matutu Chacha amesema
wamefurahishwa na utayari wa Mkoa wa Simiyu
juu ya kuwawezesha wakulima na Benki hiyo iko tayari kutoa mikopo pia kwa
wakulima wa zao la pamba ambao wanazalisha zaidi ya asilimia 60 ya pamba yote
nchini ili izalishwe kwa wingi zaidi na katika ubora wa hali ya juu.
Chacha amesema wataalam wa kilimo wa
Mkoa wa Simiyu kwa kushirikiana na wataalam wa benki ya
Maendeleo ya kilimo Tanzania (TADB) watakutana ili kuona namna watakavyofanya
kazi kwa pamoja ili mikopo itakayotolewa iweze kuwa wa manufaa kwa wakulima na
nchi kwa ujumla.
Aidha amewaeleza Wakurugenzi wa
Halmashauri zote kuwa, Halmashauri zinaweza kupatiwa mikopo ili ziweze
kuendesha miradi ya kilimo itakayoweza kuwa
vyanzo vipya vya mapato kwa Halmashauri zao.
Mkuu wa Mkoa wa Simiyu Mhe. Anthony Mtaka, akizungumza ofisini kwake na uongozi wa TADB
COMMENTS