Naibu Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, Eng. Edwin Ngonyani, akizungumza na wananchi wa kata ya Chilonwa, wilayani Ch...
Naibu Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi
na Mawasiliano, Eng. Edwin Ngonyani, akizungumza na wananchi wa kata ya
Chilonwa, wilayani Chamwino mkoani Dodoma leo mara baada ya kukagua
daraja la Chilonwa lililopo mkoani humo.
Naibu Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi
na Mawasiliano, Eng. Edwin Ngonyani, akisalimia wananchi wa kata ya
Chilonwa, wilayani Chamwino mkoani Dodoma alipotembelea wilayani hapo
leo, ikiwa ni kutekeleza ahadi yake ya kukagua daraja la Chilonwa kwa
Mbunge wa jimbo la Chilonwa, Mhe. Joel Makanyaga.
Mbunge wa jimbo la Chilonwa, Mhe.
Joel Makanyaga, akifafanua jambo kwa Naibu Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi
na Mawasiliano, Eng. Edwin Ngonyani (kushoto kwa Mbunge), alipofika
jimboni hapo kukagua daraja la Chilonwa, wilayani Chamwino mkoani Dodoma
leo.
Muonekano wa Daraja la Chilonwa
lililopo kata ya Chilonwa, wilayani Chamwino mkoani Dodoma. Daraja hilo
ni kiungo kati ya mkoa wa Dodoma, Manyara na Arusha.
Sehemu ya daraja la Chilonwa
iliyoathirika kutokana na shughuli za kibinaadamu kama vile kilimo na
hivyo kupelekea kwa daraja hilo kufukiwa na mchanga na kuwa fupi.
………………………………………………………………..
Wananchi wa kata ya Chilonwa,
wilaya Chamwino mkoani Dodoma wameiomba Serikali kuchukua hatua za
haraka kujenga daraja la Chilonwa lililopo katika kata hiyo ili kutatua
kero ya usafiri kwa wananchi hao na maeneo jirani hususan katika
kipindi cha masika.
Wakieleza kero yao kwa Naibu Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na
Mawasiliano Eng. Edwin Ngonyani, wananchi hao wamesema wanaamini kuwa
ujio wa Naibu Waziri huyo katika kata yao kutaleta ufumbuzi wa kero
hiyo.
“Tunaamini sasa tutapata mwarobaini wa daraja hili kwani
tatizo hili ni la muda mrefu, siku hadi siku daraja linakuwa fupi
kutokana na kufukiwa na mchanga na hivyo hupelekea maji kujaa darajani
hapa kipindi cha masika na watu kushindwa kuvuka”, amesema mmoja wa
wananchi hao.
Aidha, wananchi hao wamemwomba
Naibu Waziri huyo kurekebisha daraja hilo kwa kulijenga juu zaidi ili
kupitisha maji na kupitika katika vipindi vyote vya mwaka kutokana na
kwamba lililopo sasa lipo chini zaidi mara baada ya kufukiwa na mchanga.
Wananchi hao wameeleza masikitiko
yao kwa Naibu Waziri huyo hususan katika kipindi cha masika ambapo
wamesema hutumia kiasi cha shilingi elfu kumi kuvushwa kutoka sehemu
moja kwenda nyingine na wengine hupoteza maisha wakiwa wanavuka.
Sambamba na hilo wananchi hao
wamependekeza kuwa ujenzi wa daraja hilo uhusishe wataalamu waliobobea
na ambao watahakikisha daraja hilo linakamilika mapema na kwa viwango.
Kwa upande wake Naibu Waziri
Ngonyani, amewataka wananchi hao kuacha tabia ya kufanya shughuli za
kibinaadamu kama kilimo katika njia ya mto kwani hali hiyo hupelekea
udongo kumung’unyuka na hatimaye mchanga kufunika daraja.
Amemtaka Mbunge wa jimbo la
Chilonwa, Mhe. Joel Makanyaga, kwa kushirikiana na viongozi wa kata na
kijiji kuhamasisha wananchi kuacha kufanya shughuli za kibinaadamu kando
ya mto.
Amefafanua kuwa Wizara yake
kupitia Wakala wa Barabara (TANROADS), mkoani Dodoma itahakikisha
kwanza ina utengeneza mto huo kwa kuelekeza maji yote katika mto.
Naye, Mbunge wa jimbo la
Chilonwa, Mhe. Joel Makanyaga, amempongeza Naibu Waziri huyo kwa
kutembelea jimboni hapo na kuahidi kuwasimamia wananchi wake katika
kulinda miundombinu hiyo.
Naibu Waziri Ngonyani leo
ametembelea na kukagua Daraja la Chilonwa, wilayani Chamwino mkoani
Dodoma ikiwa ni kutekeleza ahadi yake ya kutembelea na kukagua daraja
hilo kwa Mbunge wa jimbo la Chilonwa, Mhe. Joel Makanyaga.
COMMENTS