NA IMMACULATE MAKILIKA- MAELEZO Umoja wa Wavunaji Sao Hill (UWASA) pamoja na Wadau wa mazao ya miti wamepong...
NA IMMACULATE MAKILIKA- MAELEZO
Umoja wa Wavunaji Sao Hill (UWASA) pamoja na Wadau wa mazao ya
miti wamepongeza jitihada za Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania John Pombe
Magufuli za ugawaji wa malighafi za misitu kwa wenye viwanda vya
mbao.
Akizungumza na waandishi wa habari leo jijini Dar es
salaam, Mwenyekiti wa UWASA, Christian Ahia pamoja na wadau wa mazao ya
miti wamesema kuwa hatua hiyo itawasaidia katika kuboresha
na kupanua soko la mbao hapa nchini.
“Tunaipongeza serikali kwa hatua nzuri iliyofikia
ambapo imetoa vibali 421 kwa wawekezaji wa viwanda vya kuchakata
mbao huko Mafindi mkoani Iringa, ukilinganisha na vibali
1,000 vilivyokuwa vimetolewa awali kwa watu ambao hawakuwa na
wawekezaji halali wa mbao” alisema Ahia.
Naye, Katibu Mkuu wa UWASA, Dkt. Bazil
Tweve alisema kuwa, serikali ina misitu zaidi ya 15 nchi
nzima, ambapo msitu wa Sao hill unazalisha asilimia
95 ya mbao zote zinazotumika nchini, hali ambayo
ilisababisha uhaba wa malighafi katika viwanda vya kuchakata mbao kwa vile
baadhi ya wavunaji hawakuwa na sifa na vigezo vya kufanya shughuli hiyo.
“Serikali ilifanya upembuzi yakinifu na kutoa vibali 421 kwa
viwanda vya kuchakata mbao, tunaishukuru serikali na kuipongeza kwa hatua hii
muhimu ya kuona tija ya viwanda na sisi tunaahidi kufanya shughuli zetu kwa
kufuata taratibu na sheria zilizowekwa alisema Dkt Tweve.
Hapo awali kabla ya upembuzi yakinifu wa kubaini wawekezaji halali
wa kuchakata mbao, kulikuwa na uhaba wa malighafi ambao ulisababishwa na
utaratibu usiofaa wa ugawaji wa malighafi hizo.
Licha ya pongezi hizo kwa serikali UWASA imesema inakabiliwa na
changamoto za masoko ya mbao zinazochakatwa nchini, na hivyo wameiomba serikali
kuwasaidia kutafuta soko ndani na nje ya nchi kwa ajili ya kuuza bidha zao.
Aidha, changamoto nyingine inayowakabili UWASA ni kiwango kikubwa
cha kodi zinazotozwa na Mamlaka ya Mapato (TRA) pamoja na Halmashauri ambapo
wameziomba Mamlaka husika kuwapunguzia kiwango cha kulipa tozo hizo.
COMMENTS