Benny Mwaipaja, WFM Serikali imesema inaendelea kupitia sheria, kanuni na taratibu za misamaha ya kodi mwaka hadi mwaka ili k...
Benny Mwaipaja, WFM
Serikali
imesema inaendelea kupitia sheria, kanuni na taratibu za misamaha ya
kodi mwaka hadi mwaka ili kuhakikisha kuwa misamaha yote isiyokuwa na
tija inafutwa na hivyo kuiwezesha Serikali kuongeza mapato kwa ajili ya
kupeleka huduma za maendeleo kwa wananchi wake.
Kauli
hiyo imetolewa Bungeni Mjini Dodoma na Naibu Waziri wa Fedha na Mipango,
Mhe. Dkt. Ashatu Kijaji (Mb), alipokuwa akijibu swali la Msingi la
Mbunge wa Masasi, Mhe. Rashid Mohamed Chuachua (CCM), aliyetaka kujua
namna Serikali inavyodhibiti misamaha ya kodi tangu irekodiwe kwa
viwango vya juu Mwaka wa Fedha 2011/2012.
Mhe.
Chuwachuwa alihoji mwenendo wa utoaji wa misamaha ya kodi kwa wawekezaji
kwa maelezo kuwa Tanzania imekuwa miongoni mwa nchi zilizopoteza fedha
nyingi kwa ajili ya misamaha ya kodi ikilinganishwa na nchi nyingine za
Afrika Mashariki kwa kigezo cha kuvutia Wawekezaji.
Alisema
kuwa kwa mujibu taarifa ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za
Serikali ya mwaka 2009-2010, Tanzania ilipoteza asilimia 15 ya Pato la
Taifa lililotarajiwa kukusanywa kutokana na misamaha ya kodi, mwaka
2010-2011 asilimia 8, kwa mwaka 2011-2012 asilimia 27 ya mapato ya
Serikali yalipotea.
“Je hali ya misamaha ya kodi kuanzia 2013-2014 hadi sasa ikoje’’. Alihoji Mhe. Chuachua.
Akijibu
swali hilo Naibu Waziri wa Fedha na Mipango, Mhe. Dkt. Ashatu Kijaji
(Mb),misamaha ya kodi kama sehemu ya asilimia ya Pato la Taifa katika
kipindi cha kuanzia mwaka 2013/14 hadi sasa imekuwa ikipungua mwaka hadi
mwaka.
“Misamaha
hiyo ilikuwa asilimia 2.2 ya Pato la Taifa mwaka 2013/14, asilimia 1.9
ya Pato la Taifa katika mwaka 2014/15 na asilimia 1.1 ya Pato la Taifa
katika mwaka 2015/16” Alifafanua Dkt. Kijaji.
Aidha
aliongeza kuwa misamaha ya kodi ikilinganishwa na mapato ya kodi imekuwa
ikipungua kutoka asilimia 18 ya mwaka 2013-2014 hadi kufikia asilimia
8.6 ya mapato yote ya kodi katika mwaka 2015-2016.
Dkt.
Kijaji alifafanua kuwa misamaha ya kodi inatolewa na Serikali kwa mujibu
wa sheria, kanuni na taratibu za kodi zilizopo, huku kukiwa na baadhi
ya huduma zinazotolewa katika jamii ambazo hazistahili kulipiwa kodi kwa
sababu hazina manufaa ya kibiashara.
‘’Pamoja
na hatua nzuri zinazochukuliwa na Serikali za kupunguza misamaha ya
kodi ni vema ikafahamika kwamba si kila msamaha wa kodi una madhara hasi
katika jamii na uchumi kwa ujumla’’. Alisema Dkt. Kijaji.
Alitolea
mfano wa mashirika ya dini yanayopata misamaha ya kodi kwa mujibu wa
Sheria ya Kodi ya Ongezeko la Thamani (VAT) (2014), kwa sababu huduma
zinazotolewa na taasisi hizo hazina faida ya kibiashara kama ilivyo kwa
kampuni za kibiashara.
Katika swali la nyongeza Mbunge huyo, alitaka kujua mpango wa Serikali kuhusu misamaha ya kodi kwa mwaka wa fedha 2017-2018.
Akijibu
swali hilo la nyongeza Naibu Waziri wa Fedha na Mipango, Mhe. Dkt.
Kijaji, alimuomba Mhe. Chuachua awe na subira hadi tarehe 8 mwezi huu
ambapo Serikali itapeleka mapendekezo yote katika Bunge, ili mapendekezo
hayo yaweze kujadiliwa na kupitishwa na Bunge.
COMMENTS