NA BALTAZAR MASHAKA, MWANZA KAMISHNA Mkuu wa Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) Charles Kichere amewahamasisha wananchi wenye maj...
NA BALTAZAR MASHAKA, MWANZA
KAMISHNA
Mkuu wa Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) Charles Kichere amewahamasisha
wananchi wenye majengo katika Jiji la Mwanza kuhakikisha wanalipa kodi
ya majengo kwa wakati ili kuepuka kutozwa faini au kufikishwa
mahakamani.
Akizungumza
na waandishi wa habari pamoja na wadau wa kodi jijini Mwanza jana
Kichere alisema kodi ya majengo ipo kwa mujibu wa sheria na italipwa
mara moja kwa mwaka, hivyo ni muhimu wananchi wakailipa mwaka huu wa
fedha kabla ya Juni 30 .
Alisema
TRA haina sababu ya kufikishana mahakamani an wananchi lakini
watakaoshindwa kulipa ndani ya muda wa kisheria watalazimika kulipa na
tozo au kufikishwa mahakamani na kulingana na matakwa ya sheria za
mamlaka hiyo watalipa sh. 70,000 badala ya viwango vya sh. 20,000
(Nyamagana) na sh. 15,000 (Ilemela) vya sasa.
“ TRA
na Serikali ya Mkoa wa Mwanza inalenga kuwaelimisha na kuwahamasisha
wananchi kulipa kodi hii bila adhabu ifikapo Juni 30, mwaka huu ambayo
ni mwisho.Wenye majengo kwenye Halmashauri ya Jiji na Manispaa ya
Ilemela ambao hawajapokea Ankara zao za kodi wakazichuke ofisi za TRA au
kwa viongozi wa serikali za mitaa yao ama wajisajili na kulipia benki
yoyote ya biashara,”alisema Kichere.
Alisema
TRA mkoa wa Mwanza inasimamia kodi ya majengo yaliyokamilika na
kutumika kwa makazi na biashara yaliyothaminishwa au la,yaliyopimwa na
yasiyopimwa katika Halmashauri ya Jiji la Mwanza pamoja na Manispaa ya
Ilemela.
Alieleza
kuwa nyumba zilizothaminiwa wamiliki watalipa kodi kwa asilimia ya
thamani ya jengo na nyumba za maeneo yasiyopimwa na ambazo
hazijathaminiwa kodi italipwa kwa viwango maalumu vilivyopitishwa na
mabaraza ya madiwani na kutangazwa na TRA kwenye vyombo vya habari.
Kamishna
mkuu huyo wa TRA alifafanua kuwa baadhi ya majengo ya serikali pamoja
na ya ibada yamesamehewa, pia wastaafu au wazee wenye umri wa miaka
60,walemavu kwa nyumba moja wanazoishi lakini zisiwe zinatumika kwa
biashara nao wamesamehewa.
Hata
hivyo aliwaondoa hofu Wakuu wa Wilaya, Naibu Meya pamoja Wakurugenzi wa
Jiji na Manispaa ya Ilemela kuwa kodi hiyo si mali ya TRA ni mali ya
halmashauri za miji, majiji na serikali za mitaa na hivyo baada ya
kukusanywa itarejesha kwenye halmashauri zikatekeleze shughuli za
maendeleo.
Kichere
alieleza zaidi kuwa ushirikiano wa serikali ya mkoa, serikali za mitaa,
umewezesha kutoa makadirio sahihi ya tozo, viwango rafiki, kuimarisha
usimamizi na ufuatiliaji, kutoa elimu kwa jamii, kushughulikia pingamizi
za kodi ya majengo kwa wakati pamoja na kuendelea kuimarisha uthamini
wa majengo.
Naye
Mkuu wa Mkoa wa Mwanza John Mongella alisema jukumu la kulipa kodi ya
serikali ambayo inawezesha kujengwa kwa barabara na huduma zingine za
jamii ni la wananchi ambapo TRA wanafanya kazi ya kuikusanya kwa dhamana
waliyopewa na serikali.
“ Dar
es Salaam wanatuzidi kwa historia tu.Kulipa na kukusanya kodi ya
serikali za mitaa kwa uadilifu tukifanya hivyo nchi yetu
itakwenda.Kwenye mkoa wangu nimeagiza hakuna mkurugenzi wa halmashauri
kutoka nje hadi amekusanya kodi tuliyokubaliana kisha tupigiane hesabu
na tuelewane,” alisema Mongella.
TRA
inasimamia na kukusanya kodi ya Majengo kuanzia Julai 2016 kutokana na
Sheria ya Fedha ya Serikali Mitaa Sura 290, Sheria ya Miji Sura ya 298
na Sheria za Mamlaka ya Mapato Tanzania sura 339.
Mkuu wa Mkoa wa Mwanza John Mongella akizungumzia umuhimu kodi ya majengo kwenye mkutano wa wadau wa kodi uliofanyika Ukumbi wa Ofisi yake.Kulia kwake ni Kamishna wa Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) Charles Kichere, Katibu Tawala wa Mkoa wa Mwanza Kamishna wa Polisi Cloudwing Mtweve na wa kwanza kulia ni Richard Kayombo Mkurugenzi wa Huduma na Elimu kwa Mlipa Kodi makao makuu TRA.Picha zote na BALTAZAR MASHAKA
Mkuu wa mkoa wa Mwanza John Mongella akielezea umuhimu wa wananchi kulipa kodi ya majengo kwenye mkutano wa wadau wa kodi uliofanyika katika Ukumbi wa Ofisi yake.Kulia kwake ni Kamishna wa Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) Charles Kichere, Katibu Tawala wa Mkoa wa Mwanza Kamishna wa Polisi Cloudwing Mtweve na wa kwanza kulia ni Richard Kayombo Mkurugenzi wa Huduma na Elimu kwa Mlipa Kodi makao makuu TRA.
Kamishna Mkuu wa Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) Charles E. Kichere akizungumza na wadau wa kodi pamoja na waandishi wa habari jijini Mwanza kuhamasisha ulipaji kodi ya majengo kwa wakati bila shuruti.Watatu kutoka kulia ni Mkuu wa Mkoa wa Mwanza John Mongella, Katibu Tawala mkoa, CP Cloudwing Mtweve (wa pili kulia) naRichard Kayombo,Mkurugenzi wa Huduma na Elimu kwa Mlipa Kodi makao makuu TRA wa kwanza kulia , kushoto wa kwanza ni Ernest Dundee,Meneja wa mamlaka hiyo mkoani humu.
COMMENTS