Na Benjamin Sawe. Mfuko wa Fidia kwa Wafanyakazi (WCF), umeendesha semina ya siku moja kwa waajiri nchini ili kutoa elimu juu ya sh...
Na Benjamin Sawe.
Mfuko wa Fidia kwa Wafanyakazi (WCF), umeendesha semina ya siku moja kwa waajiri nchini ili kutoa elimu juu ya shughuli za Mfuko na wajibu wa waajiri kwa wafanyakazi wao katika kujisajili na kuwalipa michango kwa niaba ya waajiriwa wao.
Akizungumza katika semina hiyo Makamu Mwenyekiti wa Bodi ya Mfuko huo Radhimana Mbilinyi amesema kuanzishwa kwa mfuko huo kumekuja wakati muafaka ambapo Tanzania inaelekea katika uchumi wa viwanda hivyo kupelekea ongezeko la wafanyakazi ambapo chombo hicho ndio mkombozi wa majanga yatokanayo na kazi.
“Ni muda muafaka kwa waajiri kutambua wajibu wenu katika Mfuko huu na pia kutambua madhara ya kutotekeleza wajibu wenu” Alisema Radhimina Mbilinyi.
Katika hotuba yake, Bi Mbilinyi alieleza umuhimu wa waajiri kuwalipia michango wafanyakazi wake kama sheria inavyotaka, ili kuwawekea akiba pindi wapatapo na majanga wakiwa kazini.
Akizungumza wakati akitoa mada Afisa Matekelezo Bi. Amina Likungwala amesema, Mfuko umeamua kuandaa semina hiyo ili kutoa elimu zaidi kwa waajiri kwa kutambua kuwa waajiri ndio wadau wakuu wa Mfuko huo na semina hiyo itawasaidia kujua kazi za Mfuko lakini pia wajibu wa waajiri kwa wafanyakazi katika kutoa michango ya kila mwezi.
Naye, Afisa Madai wa Mfuko huo, Grace Tarimo, alisema, Mfuko huo upo kisheria ili kutoa fidia kwa wafanyakazi watakaoumia, kuugua ama kufariki kutokana na kazi.
Mfuko wa Fidia kwa wafanyakazi ni Taasisi ya Serikali chini ya Ofisi ya Waziri Mkuu na umeundwa kwa mujibu wa kifungu cha 5 cha Sheria ya Fidia kwa wafanyakazi Sura ya 263 iliyorejewa Disemba, Mwaka 2015.
COMMENTS