JAMHURI YA MUUNGANO WA TANZANIA OFISI YA WAZIRI MKUU Simu: +255-26-232-2484/232-4560 Bar...
JAMHURI YA MUUNGANO WA TANZANIA
OFISI YA WAZIRI MKUU
Simu: +255-26-232-2484/232-4560 Barabara ya Reli na Mahakama,
Nukushi: +255-26-232-1955, S. L. P. 980,
24 Aprili, 2017
TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI
WAZIRI MKUU AKAGUA MAANDALIZI YA SHEREHE ZA MUUNGANO
WAZIRI MKUU Kassim Majaliwa amefanya ukaguzi wa miundombinu kwa ajili ya sherehe za miaka 53 ya Muungano wa Tanganyika na Zanzibar na kusema kuwa maandalizi yake yako pazuri.
Waziri Mkuu ametoa kauli hiyo leo mchana (Jumatatu, Aprili 24, 2017) mara baada ya kupokea taarifa ya maandalizi na kukagua Uwanja wa Jamhuri ambapo sherehe hizo zitafanyika na uwanja wa Nyerere Square ambako zitafanyika burudani mbalimbali kama sehemu ya maadhimisho hayo.
“Nilikuja kuangalia maandalizi ya sherehe hizo yamefikia wapi, najua kutakuwa na maonyesho ya kijeshi zikiwemo michezo na burudani kutoka Tanzania Bara za Visiwani,” alisema.
Waziri Mkuu alitumia fursa hiyo kuwakaribisha wakazi kutoka wilaya zote za mkoa wa Dodoma na mikoa ya jirani wafike kwenye maonyesho hayo ambayo kwa mara ya kwanza katika historia ya Tanzania yanafanyika mkoani humo.
“Tunatarajia wageni wengi kutoka nje ya mkoa huu wakiwemo viongozi wastaafu wa kitaifa, waheshimiwa mabalozi na wake wa waasisi wa Taifa hili, Mama Maria Nyerere na Mama Fatma Karume. Pia tutawatambulisha rasmi ndugu zetu waliochanganya udongo wa Tanganyika na Zanzibar mwaka 1964,” alisema.
Kwa upande wake, Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge, Kazi, Vijana, Ajira na Watu Wenye Ulemavu), Mhe. Jenista Mhagama alimhakikishia Waziri Mkuu kwamba sehemu zilizobakia zitakamilika kabla ya kesho.
IMETOLEWA NA:
OFISI YA WAZIRI MKUU,
S. L. P. 980,
DODOMA.
JUMATATU, APRILI 24, 2017.
COMMENTS