JAMHURI YA MUUNGANO WA TANZANIA WIZARA YA NISHATI NA MADINI Telegramu "NISHATI" ...
JAMHURI YA MUUNGANO WA TANZANIA
WIZARA YA NISHATI NA MADINI
Telegramu "NISHATI" Barabara ya Kikuyu,
Simu: +255 26 2322017 S. L. P. 422,
Nukshi: +255 26 2320148 40474 DODOMA.
Barua Pepe: ps@mem.go.tz
TAARIFA KWA UMMA
MAONESHO YA 6 YA KIMATAIFA YA MADINI YA VITO ARUSHA, TAREHE 3-5 MEI, 2017
Wizara ya Nishati na Madini kwa kushirikiana na Chama cha Wafanyabiashara wa Madini Tanzania (TAMIDA), wameandaa Maonesho ya 6 ya Kimataifa ya Madini ya Vito ya Arusha (AGF), yatakayofanyika kuanzia tarehe 3 hadi 5 Mei, 2017 katika Hoteli ya Mount Meru, jijini Arusha.
Maonesho hayo yanayotarajia kuwakutanisha washiriki (exhibitors) zaidi ya 100 kutoka nchi za Afrika Mashariki, Kati na Kusini na wanunuzi wa kimataifa zaidi ya 1000 pamoja na wadau mahiri wa tasnia ya vito, yanalenga kuendeleza azma ya kuifanya Arusha kuwa kitovu cha Madini ya Vito Afrika. Pia, yanadhamiria kuendeleza biashara ya madini ya vito katika nchi za kusini mwa Jangwa la Sahara.
Ili kuwezesha azma hiyo kufikiwa, Wizara ya Nishati na Madini na TAMIDA, wanachukua fursa hii kuwaalika wadau wote wa Sekta ya Madini na wamiliki wa leseni za biashara ya madini, Masonara na wachimbaji wakubwa na wadogo wa madini ya vito kushiriki kwenye Maonesho hayo.
Mabanda ya maonesho yanapatikana kwa gharama za Dola za Marekani 1,000. Kamati ya Maonesho itasimamia ugawaji wa mabanda hayo kwa ushindani (first come-first served).
Mbali na Maonesho, kutakuwepo na Mnada wa Serikali kwa Madini ya Tanzanite na Madini mengine ikiwa ni pamoja na bidhaa za Usonara kama vile mikufu, pete na hereni.
Aidha, kutokana na hilo, Wizara haitatoa vibali vyovyote vya kusafirisha madini ya vito nje ya nchi wiki moja kabla ya maonesho na katika kipindi cha wiki mbili baada ya maonesho ili kuhakikisha kunakuwepo na madini ya vito ya kutosha kwenye maonesho hayo.
Taarifa zaidi kuhusu usajili zinapatikana katika Ofisi za Madini za Kanda zilizo katika Miji ya Arusha, Mwanza, Dar es salaam, Mtwara, Mpanda, Shinyanga, Mbeya, Musoma, Songea na Singida au Ofisi za TAMIDA. Wanunuzi wanatakiwa kujisajili kupitia tovuti ya maonesho: www.arushagemshow.com; au kwa barua pepe ya maonesho: info@arushagemshow.com; au kwa njia ya simu zifuatazo 0786366968, 0767498869 na 0767223387.
Imetolewa na;
Kitengo cha Mawasiliano Serikalini
Aprili 28,2017
COMMENTS