Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Kassim Majaliwa akipokea Medali ya Dhahabu kutoka kwa Mwanariadha wa Tanzania Alph...
Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, leo
limezizima kwa nderemo na shangwe pale alipotambulishwa rasmi
mwanariadha Alphonce Simbu, Mshindi wa medali ya dhahabu wa Mumbai
Marathon, na moja ya washindi wa London Maratho
Mwanariadha huyo ambaye pia ni balozi maalum wa
DStv, alilitembelea Bunge kama mgeni maalum wa Waziri wa Habari,
Utamaduni na Michezo Harison Mwakyembe akiambatana na muwakilishi wa
DStv Johnson Mshana na maafisa kadhaa waandamizi wa Jeshi
la kujenga Taifa akiwemo Kanali K.J Mziray – Mkuu wa Utawala na Mafunzo
wa JKT
Mara baada ya naibu spika wa Bunge Dk. Tulia Akson
kumtaja Simbu, bunge lilizizima kwa shangwe kwa muda hali iliyoashiria
kuraha kubwa kwa wabunge kuweza kumshuhudia mwanariadha huyo ambaye ni
tegemeo kubwa la Tanzania katika mashindano
ya riadha ya Dunia yatakayofanyika mwezi Agosti mwaka huu jijini
London.
Baada ya ziara hiyo, Simbu alipata fursa ya
kusalimiana na Waziri mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Kassim
Majaliwa na kisha kuwa na mazungumzo mafupi na Waziri Mwakyembe.
Akiongea wakati wa kupiga picha ya pamoja na Simbu,
Waziri mkuu Kassim Majaliwa alimpongeza sana mwanariadha huyo na kusema
kuwa Serikali inatambua na kuthamini sana jitihada zilizofanywa na
wadau wote katika kufanikisha ushindi wa Simbu.
Pia alimtakia kila la heri katika maandalizi na kisha ushiriki wake
katika mashindano ya Dunia yanayomkabili mwishoni mwa mwaka huu.
Naye Waziri mwenye dhamana ya Michezo Harison
Mwakyembe ambaye ndiye aliyemualika Simbu Bungeni, alisema kuwa wizara
imekuwa ikishirikiana na wadau kwa karibu ambapo hata wakati wa Safari
ya Simbu kwenda London, wizara ilihakikisha safari
hiyo inafanikiwa. Ameonyesha kufurahishwa kwake na vipaji vilivyopo na
kusema nguvu za ziada zitawekwa ili kuhakikisha kuwa vipaji hivyo
vinaibuliwa na kukuzwa kwa manufaa ya taifa zima.
Kwa upande wake, Simbu alisema kitendo cha yeye
kualikwa bungeni kimempa faraja kubwa na pia alifurahi sana kuona jinsi
wabunge walivyomshangilia na kumpongeza. “Kwakweli ujio wangu bungeni
umenipa faraja kubwa kuona ni jinsi gani wabunge
wote walivyofurahishwa na mafanikio niliyopata na sifa niliyoiletea
nchi. Hii imenipa sana moyo na uzalendo kwani ni dhahiri kuwa taifa zima
liko nyuma yangu na linanunga mkono kikamilifu” alisema Simbu
Alitoa shukrani za pekee kwa wadhamini wake DStv,
pamoja na Waziri Mwakyembe kwa jitihada kubwa anazofanya. Amesema
anaamini kwa mwenendo huu yeye, wanariadha wengine na wanamichezo wote
wa Tanzania watafika mbali na hatimaye Tanzania itakuwa
kinara katika ulingo wa michezo duniani. Pia alilishukuru Jeshi la
Kujenga Taifa JKT kwa kumruhusu kufanya mazoezi na kushiriki katika
mashindano mbalimbali.
Simbu ambaye ni miongoni mwa wanariadha bora wa
Tanzania alivunja rekodi yake aliyoiweka mwaka jana nchini Japan ya muda
wa 2:09:19 na hatimaye katika mashindano ya London Marathon mwaka huu
alitumia muda wa 2:09:10 ambao ndio muda wake
bora zaidi.
Simbu ni miongoni wa wachezaji wa timu ya taifa ya riadha watakaoshiriki mbio za Dunia mwezi Agosti mwaka huu jijini London.
COMMENTS