TANGAZO KWA WATANZANIA WOTE NA WALE WANAOISHI NJE YA NCHI (DIASPORA) Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kupitia Wiz...
TANGAZO KWA WATANZANIA WOTE NA WALE WANAOISHI NJE YA NCHI (DIASPORA)
Serikali
ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kupitia Wizara ya Mambo ya Nje na
Ushirikiano wa Afrika Mashariki, inaendelea na jitihada zake za
kuhamasisha Watanzania wanaoishi nje ya nchi (Diaspora) katika kuchangia
maendeleo ya nchi yao. Ili kufanikisha hilo, Wizara kwa kushirikiana na
wadau mbalimbali wa maendeleo imekuwa ikizishawishi taasisi mbalimbali
hapa nchini kutoa huduma na fursa za biashara na uwekezaji, ambazo
zitasaidia Diaspora kuwekeza kiurahisi hapa nchini. Juhudi hizi ambazo
zilianza tokea Serikali ya Awamu ya Nne zimeanza kutoa matunda makubwa
ambapo thamani ya uwekezaji kutoka kwa Diaspora inaongezeka kila
kukicha.
Kutokana
na umuhimu wa Diaspora katika kuchangia maendeleo ya nchi na huduma
nyingine za kijamii; Serikali inapenda kutumia nafasi hii kuwakumbusha
Watanzania wote wanaoishi nje ya nchi (Diaspora) umuhimu wa kuheshimu na
kutii sheria na taratibu katika nchi wanazoishi. Aidha, Serikali pia
inapenda kuwakumbusha tena Watanzania wote wenye nia ya kusafiri nje ya
nchi kwa lengo la kupata ajira au kutafuta maisha bora (greenpastures),
kuhakikisha kuwa mikataba ya ajira inatambulika na mamlaka za nchi
husika. Sambamba na hilo, Wizara ya Mambo ya Nje na Ofisi za Balozi za
Tanzania nje ya nchi zitaendelea kuwa mstari wa mbele kusaidia kutatua
matatizo ya namna hiyo kwa Watanzania; pamoja na Taasisi za Serikali
kama vile Wakala wa Ajira Tanzania (TAESA).
Serikali
pia inawakumbusha Watanzania wanaotaka kusafiri nje ya nchi kwa malengo
mbalimbali kama vile masomo, biashara, makazi au masuala yoyote binafsi
nao kuheshimu sheria na taratibu za nchi husika. Taratibu hizo ni
pamoja na:
1)
Kujitambulisha na kujiandikisha kwenye Ofisi za Balozi za Jamhuri ya
Muungano wa Tanzania katika nchi wanazoishi au kama katika nchi hizo
hakuna Ofisi ya Ubalozi wanashauriwa kuwasiliana na Ofisi za Ubalozi
zilizo karibu na nchi yao. Kufanya hivyo kutarahisisha maafisa wa
Ubalozi kuweka kumbukumbu zao kwa ajili ya mawasiliano ili kama kuna
taarifa muhimu ziwafikie kwa wakati; au endapo watapata majanga ya aina
yoyote waweze kuhudumiwa mapema;
2) Kuheshimu sheria, taratibu na kanuni za nchi wanazoishi na kuwa raia wenye uzalendo na hekima;
3)
Kutojihusisha na tabia chafu zitakazohatarisha maisha yao kama vile
kufanya biashara za magendo na madawa ya kulevya ambazo zinaweza kuwa na
madhara kwao binafsi na pia kuiletea nchi yetu sifa mbaya;
4)
Kutunza Hati za Kusafiria (pasipoti) kwa kuwa ni utambulisho muhimu kwao
na pia ni nyaraka muhimu ya Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa
Tanzania;
5)
Kutumia fursa zilizopo katika nchi wanazoishi kwa madhumuni ya kujiletea
maendeleo yao na bila kusahau kutumia ujuzi, elimu, na maarifa
waliyoyapata kwa ajili ya kuchangia kukuza uchumi wa nchi yao;
6)
Kuendelea kuitangaza Tanzania na kuwa mabalozi wazuri wenye uelewa na
upendo wa nchi yao ili kuvutia watalii na wawekezaji wengi kuja hapa
nchini;
7) Kuendeleza matumuzi ya Lugha ya Taifa ya Kiswahili popote walipo ikiwa kama sehemu ya kukuza diplomasia ya utamaduni wetu;
8)
Kuwaelimisha na kuwahimiza ndugu zao na watoto wao popote walipo huko
ughaibuni kutumia lugha ya Kiswahili na kueneza historia na tamaduni za
Kitanzania ili wasisahau walikotoka.
Tunapenda
pia kutumia nafasi hii kuwakumbusha kuwa Serikali ya Awamu ya Tano
inaendelea na jitihada zake thabiti za kutengeneza mazingira wezeshi ya
kuwatambua, kuwahamasisha na kuwashirikisha Diaspora katika kuleta
maendeleo yenye matumaini na tija kwa Tanzania. Michango ya Diaspora
katika maendeleo ya nchi kupitia sekta za kiuchumi, kibiashara, afya,
elimu, miundombinu, na nyingine ni muhimu; na inazidi kukua na hatimaye
itaipelekea Tanzania kuwa na uchumi wa kati katika miaka ya mbele.
Hivyo, Diaspora popote mlipo mnahimizwa kuzidi kushiriki kikamilifu
katika kujenga Taifa letu bora la leo na la kesho.
IDARA YA DIASPORA
WIZARA YA MAMBO YA NJE NA
USHIRIKIANO WA AFRIKA MASHARIKI
DAR ES SALAAM.
30 Juni, 2016
COMMENTS