Baadhi ya Wafanyakazi wa DAWASA jijini Dar es Salaam waliokutwa wakifanya usafi wa mazingira kutii agizo la Kufanya ...
Baadhi ya Wafanyakazi wa DAWASA jijini Dar es Salaam waliokutwa
wakifanya usafi wa mazingira kutii agizo la Kufanya Usafi kwa kila
Jumamosi ya kila mwisho wa mwezi ili kuyaweka maeneo ya Ofisi za
Malamka hiyo katika hali ya usafi.
(PICHA NA ARON MSIGWA – MAELEZO).
Baadhi ya Wakazi wa Mwananyamala wakipakia Taka walizozoa katika
mitaa yao katika gari la kuzoa Taka la Manispaa ya Kinondoni.
Baadhi ya Wafanyakazi wa DAWASA jijini Dar es Salaam waliokutwa
wakifanya usafi wa mazingira kutii agizo la Kufanya Usafi kwa kila
Jumamosi ya kila mwisho wa mwezi ili kuyaweka maeneo ya Ofisi za
Malamka hiyo katika hali ya usafi.
Baada ya usafi
NA ARON
MSIGWA-MAELEZO.
Wito umetolewa kwa Taasisi,mashirika, makampuni na watu binafsi
kuanzia ngazi ya familia kuendelea kuitumia Siku ya jumamosi ya kila mwisho wa
mwezi kufanya usafi wa mazingira, kupanda miti na kutunza vyanzo vya maji kwa
hiari bila kusubiri kushurutishwa na sheria kwa manufaa ya kizazi
cha sasa na kizazi kijacho.
Wakizungumza kwa nyakati tofauti baadhi ya wananchi wakiwemo
wafanyabiashara na wafanyakazi wa taasisi na mashirika mbalimbali
waliokuwa wakitekeleza wakifanya usafi katika maeneo mbalimbali ya jiji
la Dar es salaam leo wamesema kuwa hatua ya Serikali kuirasimisha Siku ya
jumamosi ya kila mwisho wa mwezi kuwa siku ya usafi wa mazingira
kitaifa inaweka msisitizo kuhusu jukumu la kila mwananchi kuwa mlinzi na
mwangalizi wa mazingira katika sehemu anayoishi.
Wamesema Suala la usafi wa mazingira linawahusu watu wote, hivyo
kila mwananchi anao wajibu wa kushiriki kikamilifu kufanya Usafi wa Mazingira
kwenye Makazi yake, Maeneo ya Biashara, maeneo ya Taasisi za Umma na maeneo
yenye mikusanyiko ya watu mbalimbali kama masoko na minada.
Bi. Zaituni Musa mkazi wa Mwananyamala, Kinondoni jijini Dar es
salaam aliyekuwa akisafisha mifereji eneo la mtaa anaoishi akishirikiana na
wananchi wenzake amesema kuwa suala la usafi wa mazingira ni jukumu la kila
mwananchi bila kuangalia cheo au nafasi yake katika jamii kwa kuwa kuishi
katika mazingira machafu kuna athari kubwa kiafya hususan kuchangia milipuko ya
magonjwa ikiwemo Kipindupindu.
" Suala la usafi wa mazingira linatuhusu sote, ni wakati wa
kuchukua hatua na kuacha kuishi kwa mazoea,nawaomba watanzania wenzangu tufanye
usafi bila kulazimishwa na Serikali kila mmoja atimize wajibu wake"
Amesisitiza Bi.Zaituni.
Nao baadhi ya wafanyabiashara wenye maduka eneo la
Mwananyamala na wale wa Soko la vyakula la Buguruni, Manispaa ya Ilala
waliokuwa wamefunga maduka na biashara zao kupisha muda wa kufanya usafi wa
mazingira kuanzia saa 12 hadi saa 4 asubuhi wamesema kuwa uamuzi wa Serikali
kuitangaza Jumamosi ya kila mwisho wa mwezi kuwa Siku ya Usafi wa mazingira
unatoa fursa kwao Kufanya Usafi wa mazingira katika maeneo wanayofanyia
biashara tofauti na awali.
" Watanzania wote wa Mijini na Vijijini tujenge desturi ya
kuweka mazingira yetu katika hali ya usafi wakati wote na katika jambo hili
kila mmoja wetu awe mlinzi wa kukemea watu wenye tabia za kutupa taka hovyo ili
maeneo yetu yawe katika hali ya usafi na yakuvutia wakati wote"
Amesisitiza Bw. Haule John mmoja wa wafanyabiashara hao.
Aidha, wamesisitiza kuwa ili kuyaweka maeneo mbalimbali katika
hali ya usafi Sheria ya Mazingira ya mwaka 2004 lazima itumike kwa mtu
yeyote atakayekaidi kufanya usafi siku hiyo kutozwa faini isiyopungua shilingi
elfu hamsini au kifungo cha kuanzia miezi mitatu mpaka miaka saba, faini ya
shilingi laki mbili ya papo hapo na shilingi milioni tano kwa
kampuni au taasisi itakayotupa taka hovyo atatozwa.
Ikumbukwe kuwa Desemba 23 mwaka jana, Serikali kupitia kwa Naibu
Waziri, Ofisi ya Makamu wa Rais Muungano na Mazingira Mhe.Luhaga Mpina
ilitangaza kuwa usafi wa mazingira nchi nzima utakuwa ukifanyika kila Jumamosi
ya mwisho wa mwezi.
Mhe.Mpina alisema kuwa hatua kali za kisheria zitachukuliwa
dhidi ya viongozi na watendaji wanaopuuzia kusimamia shughuli za usafi katika
siku hiyo pia kwa wananchi wanaoshindwa kufanya usafi katika maeneo yao kwa
mujibu wa sheria ya mazingira ya mwaka 2004 na kanuni zake pamoja na Sheria
ndogo.
Aidha, kabla ya jumamosi ya kila mwezi kutangazwa kuwa siku ya
Usafi nchini, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt.John Pombe Magufuli
kwa kuzingatia sheria ya Sikukuu za Kitaifa, aliamua maadhimisho ya sherehe za
Uhuru , 9 Desemba 2015 kwa upande wa Tanzania Bara yatumike kufanya usafi wa
mazingira nchi nzima na kuhamasisha watu kujituma kufanya kazi.
COMMENTS